May 18, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Wazazi watakiwa kutowaficha Watoto wenye usonji kwenye zoezi la sensa

Na Judith Ferdinand, TimesMajira Online, Mwanza

Wito umetolewa kwa wazazi wenye watoto wenye changamoto ya usonji na changamoto nyingine kuwatoa watoto wao ili wahesabiwe katika zoezi la sensa linalotarajia kufanyika Agousti 23 mwaka huu nchi nzima.

Hayo yamebainishwa na Mkurugenzi wa Living Together Foundation (Li-TAFO) Mhandisi Shangwe Mgaya,akizungumza na timesmajira online katika maadhimisho ya siku ya Mtoto wa Afrika ambayo uadhimisha kila ifikapo Juni 16 ambapo kimkoa yamefanyika uwanja wa Furahisha wilayani Ilemela mkoani Mwanza.

Amesema tukijua idadi ya watoto wenye usonji na serikali ikujua idadi ya watoto hao na wenye mahitaji mbalimbali maalumu ndipo itaboresha miundombinu ili hao watoto waweze kupatiwa huduma.

Lakini tukiwaficha hatutasaidia chochote zaidi tutazidi kuhangaika na serikali haitajua idadi ya watoto wenye changamoto na mahitaji maalumu ni kiasi gani.

“Tutokomeze ukatili kwa watoto wenye changamoto mbalimbali na pia tujiandae kuhesabiwa naamini ya kwamba wazazi mtawaficha hawa watoto na mtajitokeza kwa wingi ili watoto wajulikane ni wangapi ili serikali iandae mkakati kwa ajili ya watoto hawa waweze kupata msaada kama nchi nyingine zilizoendelea zinavyofanya,”amesema Mhandisi Shangwe.

Aidha ameeleza kuwa watoto wenye usonji wanavipaji hivyo wakiviendeleza wanaweza kupata watu wenye vipaji mbalimbali.

“Mtu mwenye usonji alifanya kitu anacho kipenda anatulia kabisa na anakuwa anajua kama watu wengine,” ameeleza Mhandisi Shangwe.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Baraza la Watoto Mkoa wa Mwanza Neema Theonest, amesema bado mazingira siyo rafiki kwa watoto wenye ulemavu kujisomea.

Kauli mbiu ya maadhimisho hayo kwa mwaka huu inasema, Tuimarishe ulinzi wa mtoto tokomeza ukatili dhidi yake jiandae kuhesabiwa” ambayo licha ya kuhimiza jamii kuimarisha ulinzi na kutokomeza ukatili kwa watoto pia inahimiza watu kujitokeza katika zoezi la sensa ambalo linasaidia serikali katika kuandaa mipango mikakati kwa ajili ya maendeleo ya taifa.

Mkurugenzi wa Li-TAFO Mhandisi Shangwe Mgaya, akizungumza na waandishi wa habari walipomtembelea banda lao katika maadhimisho ya siku ya Mtoto wa Afrika ambayo uadhimisha kila ifikapo Juni 16 ambapo kimkoa yamefanyika uwanja wa Furahisha wilayani Ilemela mkoani Mwanza.(Picha na Judith Ferdinand)