May 2, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Wanaochimba mchanga na kusababisha athari za kimazingira DSM waonywa

Na Mwandishi wetu, TimesMajira Online

Serikali ya Mkoa wa Dar es salaam kupitia kikosi kazi Cha kuratibu Usafishaji wa Mito mkoani humo kimeonya na kueleza kuwachukulia hatua Kali za kisheria wale wote wanaochimba mchanga kwenye mabonde na mito pasipo kibali.

Hayo yameelezwa na Afisa Madini Mkoa wa Dar es salaam Ally Maganga wakati wa Kikao Cha tathimini ya Shughuli ya Usafishaji wa Mito Dar es salaam kilichoketi leo kuhakikisha mabonde na mito vinakuwa katika Hali nzuri, kuondoa taka na ujenzi wa kingo.

Aidha Maganga ametoa wito kwa Watu wanaouza Mchanga kuhakikisha wanajirasimisha ili waweze kufanya Shughuli hiyo kwa Uhuru tofauti na Sasa ambapo baadhi yao wanafanya kazi kienyeji na kusababisha madhara kwa Wananchi ikiwemo uharibifu wa Makazi ya watu.

Hata hivyo amesema Mpaka Sasa zaidi ya vikundi 50 vimesajiliwa na Wakandarasi wanaotumia mashine zaidi ya 12 na kutoa wito kwa jamii Kuhifadhi na kulinda mito na mabonde kwa maslahi mapana ya nchi.

Kikao hicho kimehusisha Wajumbe mbalimbali wa kikosi kazi kutoka ofisi ya Mkuu wa Mkoa huo, NEMC, watu wa bonde, Wakandarasi wanaosafisha mito, vyama vya wapiga chepe na vikundi.

Kwa upande wake Kaimu Katibu tawala msaidizi sehemu ya uchumi na uzalishaji wa Mkoa wa Dar es salaam Dr. Elizabeth Mshote amesema Mpango wa Mkoa huo Ni kusafisha mito kwa kuondoa taka ngumu, tope, mchanga na kuwataka wasafisha mito kufuata kanuni, taratibu na sheria ili wasiweze kusababisha madhara kwa Wananchi.

Aidha Dr. Mshote amesema Mkoa kwa kushirikiana na awadau wapo katika mkakati wa Uanzishwaji wa vitalu kwenye maeneo ya Mito ili kuboresha mazingira ya Mito kwa kupanda Miti ambapo kwakuanzia wameanza na mto Mpigi.