May 18, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Wanafunzi St Mary’s waonyesha vipaji vya aina yake

Na Mwandishi Wetu, Timesmajira Online DSM

SHULE ya Msingi na Sekondari St. Marys Mbezi Beach imesema imejenga viwanja vya michezo shuleni hapo kama moja ya njia ya kuhamasisha michezo na kuibua vipaji mbalimbali vya wanafunzi.

Hayo yamesemwa na leo na Mkuu wa shule hiyo, Ntipoo Reca, wakati wa mahafali ya 22 ya shule hiyo yaliyofanyika shuleni hapo Mbezi Beach.

Katika mahafali hayo ambayo yamefanyika leo kwenye viwanja vya shule hiyo wanafunzi wa shule hiyo wameonyesha vipaji vya aina yake kwenye michezo mbalimbali.

Vipaji vilivyoonyeshwa na wanafunzi hao viliwafanya wazazi waliofika kwenye mahafali hayo kusimama mara kwa mara kuwatunza fedha kila walipofanya onesho.

Reca alisema shule hiyo imepanga muda maalum kwa wanafunzi kushiriki michezo mbalimbali kama mpira wa miguu mpira wa mikono sarakasi na skauti

“Shule pamoja na kufanya vizuri kitaaluma imeona umuhimu wa kujenga viwanja vya Volley Ball, mpira wa miguu, mpira wa kikapu sisi masuala ya michezo hatuyachukulii poa kwasababu tunafahamu kwamba michezo ni uchumi kwani wapo watu ambao wanaingiza mabilioni kupitia vipaji kwenye michezo mbalimbali,” alisema.

“Na tunaushukuru sana viongozi wa shule kwa kutuunga mkono kwenye michezo na kwenye viwanja hivi wameweka taa kubwa kama zinazotumika kwenye viwanja vikubwa vya michezo hali ambayo inasaidia wanafunzi kufanya mazoezi hata nyakati za usiku,” alisema

Mmoja wa wazazi, Anita John alielezea kufurahishwa na vipaji vilivyoonyeshwa na wanafunzi hao na kuitaka shule hiyo kuendelea kuibua vipaji vya wanafunzi kwani wako watu wengi wamefanikiwa kupitia michezo.

“Tumefurahi kuona vipaji ya wanafunzi hawa kwenye michezo mbalimbali na duniani hapa ziko njia nyingi za kufikia mafanikio kwa hiyo kuna mwanafunzi anaweza asiwe mzuri sana darasani lakini akawa na kipaji kwenye kuimba, mpira wa miguu, kikapu na vikampa mafanikio makubwa sana kwa hiyo ningependa shule zingine nazo ziwe na program za kuibua vipaji”