April 26, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Wakulima wapewa mbinu kupata masoko ya uhakika

Na Esther Macha, TimesMajira Online, Mbeya

WAKULIMA wa Mikoa ya Nyanda za juu Kusini wameshauriwa kuzingatia masoko ya mazao pamoja na bidhaa wanazozalisha kabla ya kuanza uzalishaji ili waweze kupata masoko ya uhakika.

Rai hiyo imetolewa na Msimamizi wa Taasisi ya Kilimo Trust iliyoko mkoani wa Mbeya, Robert Mwaluseke alipozungumza na Mtandao huu kwenye maonesho ya Wakulima ya Nane Nane yanayoendelea kwenye viwanja vya John Mwakangale.

Mwaluseke amesema, kupitia maonyesho hayo watahakikisha wanatoa elimu ya kutosha kwa wakulima juu ya utafutaji masoko na namna ya kujiunga kwa pamoja ili kutafuta masoko na namna ya kujiunga na kuunda ushirika wa kibiashara na wanunuzi.

Amesema, kama malengo ya Taasisi yao yanavyotaka, amedai watahakikisha wanawatafutia masoko kuimarisha na kuwaunganisha wakulima na wadau mbalimbali pamoja na kuboresha namna ya uuzaji na usambazaji wa pembejeo za kilimo na kuwandaa kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi.

“Pamoja na mambo yote hayo lakini sisi Kilimo Trust pia tunawaunganisha pamoja wakulima kwa kujiunga kwenye ushirika wa kibiashara ili kuongeza fursa za kibiashara,” amesema Mwaluseke.