May 18, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Mgombea Ubunge Jimbo la Mbarali Francis Mtega wakati wa kurudisha fomu kwa Msimamizi wa uchaguzi Jimbo la Mbarali ,Kivuma Msangi

Wagombea watakiwa kuhimiza amani na utulivu kipindi cha Kampeni

Na Esther Macha,TimesMajira,Mbeya

MSIMAMIZI wa Uchaguzi jimbo la Mbarali mkoa wa Mbeya, Kivuma Msangi amewataka Wagombea wa vyama mbalimbali vya Siasa kuwa chachu ya kuhimiza amani na utulivu katika kipindi chote cha kampeni.

Msangi ametoa kauli hiyo wakati akipokea na kudhibitisha fomu za mgombea Ubunge kupitia chama cha Mapinduzi CCM jimbo la Mbarali Francis Mtega katika ofisi za tume ya uchaguzi.

Amesema kuwa yeye kama msimamizi wa uchaguzi hata furahishwa kuona wagombea wanakuwa chanzo cha kuhamasisha vurugu na chuki zinazo weza kuwa chanzo cha kuvunja amani.

“Wagombea nawaomba sana, fanyeni kampeni za ustaarabu, zisizo gawa wananchi na kujenga chuki, kwani kwa kufanya hivyo ni kosa kubwa kisheria, na mimi kama msimamizi wa uchaguzi katika jimbo hili la Mbarali sitafurahishwa na jambo hilo” amesema Msangi.

Mgombea Ubunge Jimbo la Mbarali  (CCM) Francis Mtega, amesema kuwa kwa kushirikiana na chama chake atahakikisha anasimamia kikamilifu amani na mshikamano katika kipindi chote cha kampeni.

“Nashukuru sana chama changu kuniamini kupeperusha bendera, nitahakikisha nafuata maelekezo yote ninayopatiwa” amesema Mtega.

Katika zoezi hilo la urudishaji wa fomu, mgombea huyo ameambatana na viongozi wa chama, huku akisindikizwa na mamia ya wanachama  wa chama hicho.