May 4, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Wadau wa Mpango wa Kunusuru Kaya za Walengwa walemavu watoa maoni TASAF

Na Rose Itono

WADAU wa Kikao Kazi Cha kupokea maoni kuhusu ushirikishwaji wa Watu wenye Ulemavu Kwenye Mpango wa Kunusuru Kaya za Walengwa wameiomba TASAF kuutumia muda wa nyongeza kuwatambua walemavu walioachwa kwenye mpango wa kunusuru kaya hizo

Wakichangia maoni yao kwenye kikao hicho baadhi ya washiriki walisema ushirikishwaji wa watu wenye ulemavu kwenye mpango wa kunusuru kaya za walengwa utasaidia kuondoka kwenye utegemezi na kuweza kufanya shughuli za maendeleo kwa kujitegemea

Mwenyekiti wa Chama Cha Walemavu Tanzania (CHAWATA )Hamadi Komboza amesema uhakiki wa awali kwenye mpango huo umewaacha walengwa wengi kwenye hivyo kuna kila sababu ya kuangalia upya namna ya kuwafikia walemavu wote

“Ninaomba TASAF muutumie muda huu wa mpaka 2025 kuhakikisha kila kaya yenye mlemavu inaingia kwenye mpango huu ambao ni Maalumu wa kuzipatia ruzuku za ziada kaya zinazoishi na watu wenye ulemavu Ili ziweze kumufu baadhi ya gharama zinazotokana na kuishi na mtu mwenye ulemavu”amesema Komboza

Aidha ameongeza kuitaka TASAF kuangalia upya vigezo vilivyotumika kuwatambua walengwa kwenye kaya hizo Ili kuwezesha wote kunufaika na kuondokana na umasikini.

Naye Frank Latamani ambaye ni Mwenyekiti wa CHAMA Cha Walemavu wa Ngozi aina ya (Psoriasis) amesema TASAF imelisahau kundi hili kwani takwimu za awali zilizotolewa kwa walengwa zinaonesha hakuna mlemavu wa Ngozi wa Psoriasis aliyetambuliwa kwenye mpango

“Naionba TASAF iangalie namna ya kuyashirikisha makundi yote ya walemavu ikiwezekana fursa za ajira kwa walemavu wa Psoriasis zifanywe na watoto wa walengwa kwa kuzingatia changamoto ya ugonjwa huo,” amesema Latamani

Amesema kwa kuzingatia kundi hili la walemavu wa ngozi na umuhimu wa mpango huo Maalumu Ipo haja ya kuwashirikisha wataalamu wa afya kwani inaonekana wazi Jamii hailifahamu kundi hili

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Mfuko wa Maendeleo ya Jamii TASAF Ladislaus Mwamanga amesema watazifanyia kazi changamoto zote zilizotolewa na wadau Ili kufikia malengo ya mpango Maalumu uliowekwa kwenye mpango wa kunusuru kaya za walengwa.

Amesema TASAF itaendelea kusimamia jitihada za serikali kwenye mpango wake Maalumu wa kutoa ruzuku za ziada kwa kaya inayoishi na mtu mwenye ulemavu Ili kuweza kumufu baadhi ya gharama zinazotokana na kuishi na mtu mwenye ulemavu

Akiwasilisha taarifa ya mpango huo Meneja Masijala ya walengwa TASAF Phillipina Mmari amesema zoezi la uhakiki lilipangwa kwa awamu kuanzia mwezi February 2022 Hadi Januari 2023
na hadi Sasa takwimu za kaya 169,141 zenye watu wenye ulemavu 183,579 zimehifadhiwa kwenye kanzidata ya mpango.

Amesema uhakiki wa watu wenye ulemavu ulifanyika katika maeneo yote ya utekelezaji na kwamba jumla ya wanufaika 183,579 walithibitishwa kuwa walemavu ambapo 116,746 walibainika kuwa na kiwango Cha Juu Cha ulemavu na kuthibitishwa kuwa wanastahili kuingia kwenye mpango

Kikao hicho kiliwashirikisha wadau mbalimbali wakiwepo Wadau wa Maendeleo, Vyama Vya Watu wenye Ulemavu Tanzania Bara na Zanzibar ambapo mradi unaotekelezwa, Asasi zisizo za kiserikali na TASAF