May 5, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Viongozi tuache alama nzuri katika utendaji wetu wa kazi – DKT. BITEKO

Na Mwandishi Wetu, TimesMajira Online, Kilimanjaro

NAIBU Waziri Mkuu na Waziri wa  Nishati, Dkt. Doto Biteko ametoa wito kwa viongozi mbalimbali Serikalini kuhakikisha kuwa, kazi walizonazo wanazifanya kwa bidii kubwa na kuacha alama nzuri kwa  wananchi, hivyo ni muhimu kazi hizo zikaonekana na kufaidisha wananchi.

Amesema hayo leo  wakati alipomwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan katika Ibada Maalum ya kuaga Mwili wa Baba Askofu Mstaafu, Dkt. Erasto Kweka iliyofanyika katika Usharika wa Moshi Mjini mkoani Kilimanjaro.

Ibada hiyo Maalum ilihudhuriwa na viongozi mbalimbali akiwemo Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Jerry Silaa na Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Nurdin Babu.

“Nikitolea mfano wa Marehemu Baba Askofu Kweka ameacha alama nzuri duniani kwani ameanzisha vitu vingi ambapo hata kama ameondoka, vitu hivyo vinaendelea kuonekana na kufaidisha wengine  mfano wa enzi ya uhai wa Baba Askofu alitoa mchango mkubwa katika masuala mbalimbali ya kijamii ikiwemo kuleta usawa wa kijinsia, uanzishwaji wa miradi ya maji safi ndani na nje ya Dayosisi, Elimu, uanzishwaji wa Chama  cha Akiba na Mikopo pamoja na Benki ya Uchumi ya KKKT ambayo inawahudumia watu wote na madhehebu yote.” Amesema Dkt. Biteko

Dkt. Biteko ametoa wito kwa wananchi kuendelea kufanya kazi kwa bidii na kutokuta tamaa, akitolea mfano wa maisha ya Marehemu Baba Askofu Kweka ambaye alianza kutafuta maisha akiwa kijana mdogo baada ya kufiwa na Baba yake akiwa na umri wa miaka 14 mpaka hatua aliyofikia sasa ya mafanikio kwa Kanisa la KKKT  na watu wanapata huduma kupitia juhudi zake.

Katika hatua nyingine, Dkt. Biteko amesema kuwa,  Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Samia Suluhu Hassan anatambua mchango wa Marehemu Baba Askofu Kweka kwenye maendeleo ya Kanisa la KKKT na kwamba Serikali itauenzi mchango wake katika Sekta pia za Afya, Elimu na Maji.

Kwa upande wake, Mkuu wa Kanisa la Kiinjili na Kilutheri Tanzania (KKKT) na Askofu wa Dayosisi ya Kaskazini , Dkt. Fredrick Onaeli Shoo amesema kuwa, viongozi wa Kanisa hilo wamefarijika na uwepo wa viongozi wa Serikali waliojumuika nao kutoka siku msiba ulipotokea mpaka wakati wa Misa hiyo Maalum.

Pia ametoa pole kwa Wananchi na Serikali kufutia maafa yaliyotokea katika Wilaya ya Hanang, Mkoa wa Manyara ambapo baadhi ya wananchi wamepoteza maisha na wengine kujeruhiwa kufuatia maporomoko ya ardhi na ameeleza kuwa Kanisa linafarijika na juhudi mbalimbali zilizochukuliwa na zinazoendelea kuchukuliwa na Serikali katika kutatua changamoto katika eneo hilo, na tayari Waziri Mkuu , Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa yupo katika eneo la maafa na viongozi mbalimbali wa Serikali.

Marehemu Baba Askofu Mstaafu,  Dkt. Erasto N. Kweka alizaliwa tarehe 24 Aprili, 1934 katika Kijiji cha Mamba Uswaa wilaya ya Hai mkoa wa Kilimanjaro ambapo enzi ya uhai wake alitumika katika nyanja mbalimbali ikiwemo Ualimu, kabla ya kuingia ngazi ya Utumishi wa Kanisa.

Mwaka 1973 alichaguliwa kuwa Msaidizi wa Askofu wa Dayosisi ya Kaskazini wadhifa alioutumikia hadi mwaka 1976, ambapo mwaka mmoja baadaye alichaguliwa kuwa Askofu Mkuu wa Dayosisi ya Kaskazini na pia kukaimu nafasi ya Mkuu wa Kanisa kabla ya kustaafu kwa heshima mwaka 2004.

Marehemu Baba Askofu Mstaafu, Dkt. Kweka  alifariki Jumamosi tarehe 25 Novemba, 2025  saa 4 Asubuhi  akiwa na umri wa miaka 89.