May 18, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Upandaji bei zao la kahawa wawaibua watalaam wa kilimo

Na Esther Macha,Timesmajira Online, Mbeya

BAADA ya kupanda kwa bei ya zao la Kahawa nchini,  kutoka sh 4300 kwa kilo moja na kufikia sh. 6500 hadi 7000, mahitaji ya miche ya zao  hilo  yamekuwa makubwa ukilinganisha na uzalishaji wa miche kwa sasa  hali inayowaibua watalaam wa kilimo kuongeza kasi ya uzalishaji wa mbegu ili kukidhi mahitaji kwa wakulima.

Kwa mujibu wa Ofisa  Ubora Mwandamizi wa zao la Kahawa Kanda ya Mbeya, Gerald Mlay amesema kupanda kwa bei ya zao la kahawa nchini  ni matokeo ya  jitihada zilizofanywa na wadau wote wanaohusika na mnyororo wa thamani wa zao hilo likiwemo shirika la Cafe Africa Tanzania ambalo mbali na kusaidia kutafuta soko la uhakika lakini pia waliwajengea uwezo wakulima namna bora ya kuzalisha bidhaa hizo.

Mlay amesema kuongezeka kwa bei ya kahawa nchini   imewasaidia wakulima kumudu gharama za maisha  ikiwamo kusomesha watoto, kujenga na kufungua miradi mingine ya kujikwamua na umasikini.

Amesema kupanda kwa bei ya zao hilo kumechangiwa pia na mahitaji ya bidhaa hiyo duniani kutokana na kuzalishwa katika hali ya ubora ambao unamudu ushindani wa soko la dunia.

Alipongeza Shirika la Cafe Africa Tanzania, kuwa daraja katika ya wakulima , serikali na wadau kuwasaidia kuinua uchumi wa mkulima mmoja mmoja.
Amesema kwa sasa  uhitaji wa miche mipya ya zao la kahawa umekuwa mkubwa kutokana na faida inayopatikana  sambamba na kuongezeka kwa uzalishaji ukilinganisha na ilivyokuwa awali.

Licha ya manufaa mbalimbali tunayoyaona kwa wakulima wetu lakini bado wanakabiliwa na tatizo la kupanda kwa pembejeo za kilimo ambazo zinachangia kukwamisha jitihada za uzalishaji.

Amesema licha ya kupanda kwa pembejeo za kilimo hususani mbolea kutoa sh 69000 kwa mfuko mmoja hadi 12000 lakini pia upatikanaji wake umekuwa mgumu hivyo aliiomba serikali kuliangalia kwa jicho la karibu suala hilo.
Akifungua kikao hicho, Kaimu Katibu Tawala, Mkoa wa Mbeya, Donald Bombo amesema Shirika la Cafe Africa Tanzania kupitia mradi wa CODE P hadi kufikia  Mei 2022 wameweza kuwafikia  wakulima 11,999 ambapo kati yake 3,719  ni   wanawake  na 8,280 ni wanaume na kwamba katika kipindi cha miaka miwili kutoka 2021 hadi 2022 walikuwa na lengo la kuwafikia wakulima 12000.
Miongoni mwa wakulima wa zao  hilo, akiwamo Rashid Mwakosya kutoka  Chama cha Ushirika Amcos, Wilaya ya Rungwe mkoani Mbeya alisema licha ya bei  kupanda lakini bado gharama  kubwa za pembejeo za kilimo hususani mbolea imekuwa mwiba kwao.

Ameomba Serikali na wadau wengine wanaohusika na uzalishaji wa mbolea nchini kuangalia namna bora ya kuzalisha mbolea nchini ili kukidhi mahitaji ya wakulima  na kununua kwa gharama nafuu ukilinganisha na ilivyo sasa ambapo mfuko mmoja wa mbolea unauzwa kwa sh 12000 kutoka 69000 ambayo ilikuwa ikiuzwa awali.

Kwa upande wake, Meneja Programu kutoka Shirika la Cafe Africa Tanzania, Samora Mnyaonga amesema wakulima, maofisa ugani na wadau wengine wanaohusika  kwenye mnyororo wa thamani wa zao hilo kutoka mikoa ya Mbeya, Songwe na Ruvuma  wamekutana mkoani Mbeya kujadili kwa pamoja  masuala ya masoko, uongezaji thamani wa zao la kahawa pamoja na kuhimiza ushirikishwaji wa wanawake na vijana   katika uzalishaji wa kahawa.

Mnyaonga amesema kupitia kikao hicho  cha siku mbili  kinatoa fursa ya  kujadiliana   na kutafuta fursa za masoko  sambamba na  kufundishana mbinu bora za uzalishaji wa zao hilo.

Kaimu katibu Tawala mkoa wa Mbeya Donald Bombo akifungua mkutano wa wadau wa kahawa