April 20, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Umoja wana Rungwe watoa msaada wa mashuka 50 hospitali ya Busokelo

Na Esther Macha,Timesmajira Online,Mbeya

UMOJA wa wana Rungwe wanaoishi katika mikoa Mbalimbali wametoa msaada wa Mashuka 50 katika hospitali ya wilaya ya Busokelo Mkoani Mbeya  ili yaweze kukidhi mahitaji ya hospitali hiyo.

Akikabidhi msaada huo wa mashuka ,Mwenyekiti wa asasi isiyokuwa ya kiserikali (Rungwe Yetu )Kenny Lawrence amesema kuwa kila mwaka mwezi Desemba hukutana na kufanya mkutano mkuu na kujadili masuala
mbalimbali yanayohusu maendeleo katika wilaya hiyo na kutoa misaada kwa jamii.

Aidha Lawrence amesema kwamba wana utaratibu wa kutoa huduma kila mwaka hujikusanya kutoka mikoa mbalimbli kutoa misaada ya kimahitaji kwa wilaya hiyo mfano leo tumetoa msaada wa mashuka 50 kwa hospitali ya halmashauri ya Busokelo  pamoja na Matanki ya maji yenye ujazo wa maji lita, 5000 kwa soko la Kiwira na Tandale ili yaweze kuwasaidia wananchi  wanaofanya biashara mbali mbali katika maeneo ya masoko kutokana na changamoto ya uhaba wa maji  na pia kusaidia kujikinga na ugonjwa wa Corona.

“Sisi kwa kila mwaka huwa tuna utaratibu wa kujitoa kwa wana Rungwe na huwa tunafanya mkutano mkuu kwa ajili ya kujadili masuala ya kimaendeleo yanayohusu Rungwe yetu na  tunafanya hivi ili kuweka alama ili ndugu zetu walioko nje ya nchi waweze kurudi nyumbani  na  tuweze kushirikiana kwa  pamoja na kutatua changamoto mbali mbali za wilaya yetu ”amesema Mwenyekiti huyo.

Akipokea msaada huo wa mashuka( 50) Kaimu Mganga Mkuu wa halmashauri ya Busokelo Mkoani Mbeya , Dkt.Mayunga  Kuyeyema alishukuru kwa msaada huo  na kusema kwamba hospitali hiyo ni mpya  na kuna huduma ambazo zinaendelea na kwamba hivi karibuni hospitali hiyo itaanza upasuaji kwa upande wa  wanawake.

“Tunashukuru serikali ya jamhuri ya muungano wa Tanzania chini ya Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kutekeleza miradi yote iliyoanzishwa ikiwemo hospitali  hii ya Busokelo  kama mnavyojua kitu chochote kinavyoanzishwa kinakuwa na changamoto na kama tunavyoona wana Rungwe yetu mmeona kuwa hospitali ni mpya lazima itakuwa na mahitaji  mkaamua kuleta  msaada huu kwetu ni msaada mkubwa  sana tunashukuru sana ,unajua hospitali yetu ni mpya hivyo kuna huduma ambazo zinaendelea kutolewa “amesema Dkt.Kuyeyema .

Aidha Dkt .Kuyeyema amesema wamezoea kupata misaada kutoka nje ya nchi ,amezitaka taasisi na waau na wananchi kuwa mfano wa kuchangia huduma mbali mbali .

Akizungumzia  kuhusu mahitaji Kaimu Mganga mkuu huyo amesema kuwa vitendea kazi bado ni changamoto pamoja na rasilimali watu bado ni changamoto lakini wanashu8kuru serikali kwa jitihada ujenzi wa majengo zaidi unaendelea na hii karibuni huduma zingine zitaanza kutolewa.

Phares Mbilla ni Mwanacha wa Rungwe yetu amesema kwamba wanaamini wakiwa pamoja wanaweza kushirikiana na kutatua changamoto za wana Rungwe  kwa kuibua changamoto ambapo serikali itaona kuzipatia ufumbuzi .