May 9, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Tuzo 21 za Eagle Entertainment 2023, zatolewa Sengerema

Judith Ferdinand, Timesmajira Online

Jumla ya tuzo 21 za Eagle Entertainment 2023(Eagle Entertainment Awards 2023)zimetolewa kwa watu wa kada mbalimbali na kampuni inayojishughulisha na burudani ya Eagle Entertainment ikiwa ni mwaka wa tatu mfululizo huku ombi likitolewa kwa wadau , taasisi na kampuni kuunga mkono na kuwekeza katika tuzo hizo.

Akizungumza katika hafla ya usiku wa tuzo uliofanyika Desemba 25,2023 usiku wa sikukuu ya Krismasi iliofanyika wilayani Sengerema Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni ya Eagle Entertainment na muaandaji wa tuzo Hassan Kuku ameeleza kuwa awali walianza kama Wilaya na mwaka huu wamefanya kimkoa hivyo matarajio yake ya baadae ni kuwa za Kanda na hatimaye taifa.

Ambapo ameeleza kuwa kampuni hiyo imekuwa ikiandaa tuzo hizo sasa ni mwaka wa tatu zilianza mwaka 2021 na waliziandaa kwa kiwango cha Wilaya yao lakini kwa mwaka wa 2023 wamekuwa na mafanikio kwa kiwango kikubwa yamefanyika kwa ngazi ya kimkoa huku lengo ni kutambua mchango wa kada hizo katika jamii,kutambulisha Wilaya ya Sengerema pamoja na fursa mbalimbali kwa vijana wa Wilaya hiyo.

“Zimekuwa tofauti kwani zinatolewa kwa kada mbalimbali tofauti na tuzo nyingine ambazo zimekuwa zikijikita katika kada fulani mfano kama tuzo zinazohusu waandishi wa habari tu,pia tuzo hizi zimekuwa na changamoto mbalimbali na mafanikio kwani kila siku tunapiga hatua kwa sababu tulianza tukiwa wachache tunakwenda tunaongeza wigo wa tuzo kuwa nyingi na tumejaribu kugusa makundi ambayo mwaka jana na mwaka juzi hatukuyagusa,” ameeleza Hassan.

Ameeleza kuwa tuzo hizo zimekuwa na mchango katika jamii kwani zimeweza kuibua watu wapya kila siku huku mtarajio ni kuwa mwakani watakuwa na kitu kikubwa zaidi huku aliomba wadau,mashirika na kampuni mbalimbali kuwekeza katika tuzo hizo ili ziwe bora zaidi.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Sengerema Binuru Shekidele, ameeleza kuwa tukio lililofanywa na kampuni ya Eagle Entertainment ni jambo muhimu kwa maendeleo ya Sengerema pia linatija katika serikali.

“Tukio hili la kuibua vipaji ambavyo tunavihitaji katika kuendesha nchi yetu na vijana kuwa na ushindani wa kufanya Yale ambayo walihitaji kufanya, kampuni ya Eagle Entertainment ni chachu ya utekelezaji wa mabadiliko ambayo Halmashauri inataka kuona kwa wajasiriamali baadaya ya kuwawezesha mikopo,”ameeleza Binuru.

Naye mmoja wa washiriki wa tuzo hizo aliye ibuka Mwandishi bora wa mwaka katika kipengele cha mazingira Esther Baraka ameeleza kuwa kupitia tuzo hizo ni chachu ya kufanya vizuri na waandishi wa habari wanasehemu ya kileta mabadiliko na kufanya kazi zenye kuleta tija kwa jamii.

Miongoni mwa tuzo zilizotolewa kwa mwaka 2023 ni pamoja na tuzo za heshima,Msanii Bora wa kike, Msaani Bora kiume, Mwandishi Bora wa Habari za Mazingira, Mwandishi Bora wa Habari za Elimu,Kikundi Bora cha Ujasiriamali,Mshereheshaji Bora (MC),Dj Bora wa mwaka na nyingine nyingine.

Ambapo Esther Baraka mwandishi wa Afya Radio akijinyakulia tuzo ya Mwandishi Bora wa Habari za Mazingira kwa mwaka 2023,Daniel Makaka akijinyakulia tuzo ya Mwandishi Bora wa Habari za Mazingira kwa mwaka huu, Emmanuel Timanye akijinyakulia tuzo ya Mtangazaji Bora wa Radio,tuzo ya Msanii Bora wa mwaka wa kiume ikienda kwa Baraka da Prince.

Filamu Bora ya Mwaka ilienda kwa Nafsi,DJ Bora wa Mwaka tuzo ilienda kwa DJ John,Msaani Bora wa kike tuzo ilienda kwa Dayana,Kikundi Bora cha Ujasiriamali kwa mwaka 2023 tuzo ilienda kwa Kikundi cha Mama Helen.