May 3, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Tulia Marathon yachochea fursa za kiuchumi Mbeya

Na Esther Macha,Timesmajira,Online,Mbeya

Imeelezwa kuwa uwepo wa mbio za Tulia Marathon mkoani Mbeya zimechochea
fursa za kiuchumi kwa wafanyabishara kutokana na mwingiliano mkubwa
wa watu kutoka mikoa mbalimbali pamoja na nchi jirani ya Kenya.

Hayo yamebainishwa na Diwani wa Kata ya Majengo,Mwenyekiti wa Chama cha Riadha Mkoa wa Mbeya,Maulid Jemedali wakati akizungumza na mwandishi wa TimesMajira Online katika viwanja vya Kumbukumbu ya Sokoine jijini Mbeya ikiwa ni siku ya kwanza ya mashindano hayo.

Diwani wa kata ya Majengo ,Maulid Jemedali

Ambapo amesema kuwa Tulia Marathon imekuwa msaada mkubwa kwa wajasiliamali wa Mkoa wa Mbeya kwa kukuza uchumi.

Sanjari na hayo Jemedali amesema kuwa uwepo wa mbio hizo umekuwa chachu ya kuchangia shughuli za miradi ya maendeleo ikiwepo sekta ya elimu na
afya jambo ambalo inaongeza tija katika utoaji huduma bora kwa jamii.

“Kwa Jiji la Mbeya tunaona mambo mengi ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo katika sekta ya elimu na afya yanafanywa na fedha zinazopatikana kupitia mashindano ya mbio za Tulia Marathoni,”amesema.

Ofisa Habari na Mawasiliano wa Taasisi ya Tulia Trust,Joshua Mwakanolo amesema kuwa lengo la mbio hizo ni kuboresha miundombinu ya elimu na afya na kwamba huo ni msimu wa saba toka kuanzishwa kwa Mbeya Tulia Marathon.

Ofisa Mawasiliano wa Taasisi ya Tulia Trust ,Joshua Mwakanolo

‘’Kwa mwaka 2022 fedha iliyopatikana kwenye Mbeya Tulia Marathon ilipelekwa katika ujenzi wa mabweni ya shule ya sekondari Ipinda wilayani Kyela baada ya hapo yalijengwa madarasa mawili shule ya sekondari Lyoto pamoja na ofisi,”amesema Mwakanolo.

Hata hivyo amesema kwa mwaka huu wanategemea kuwa fedha itakayopatikana waone jinsi gani wataweza kuigawa ili
kuboresha miundombinu ya afya na elimu,kwani muitikio ni mkubwa ambapo takribani watu 4,000 waliojitokeza kati yao 14 ni kutoka nchi jirani ya Kenya.

Amesema kuwa mashindano hayo yamekuwa na mchango mkubwa sana kwa jamii hususani kuchangia ukuaji wa kipato cha mtu mmoja mmoja na vikundi wakiwemo wafanyabishara wa viatu,nguo,mama lishe na wauzaji wa vileo.

Kwa upande wake Diwani wa Viti Maalum Kata ya Makongolosi Sophia Mwanautwa, amesema kuwa lengo kuu la Tulia Marathon ni kuboresha elimu na afya hivyo Spika wa Bunge amekuwa akipenda maendeleo na akizungumzia elimu na
anafanya kwa vitendo.

Diwani wa Viti Maalum Kata ya Makongolosi wilayani Chunya Sophia Mwanauta

Mwanauta amesema kuwa wanaMbeya wanapoona Spika anafanya jambo wamuunge mkono na kumpa sapoti ili aweze kufanya vitu vya maendeleo.

‘’Kwasababu kujiandikisha sio lazima ukimbie mbio mimi hapa,nimejiandikisha nakimbia kilometa tano(5) na namba yangu ni 0368 sio,kwamba kesho nitakimbia ila nimechangia kumsapoti Spika na Mbunge wa Jimbo la Mbeya , nawaomba wana Chunya mwakani wajitokeze kwa wingi ili kumuunga mkono mwana mama huyu katika juhudi zake za kuboresha elimu kwa Mkoa wa Mbeya,’’amesema Diwani huyo.