May 9, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

TRA,Dodoma yarudisha shukrani kwa jamii

Na Zena Mohamed,Timesmajiraonline,Dodoma.

MAMLAKA ya Mapato Tanzania(TRA),Katika kuadhimisha ya kilele cha siku ya shukrani kwa mlipa kodi,Mkoa wa Dodoma wameadhimisha kwa kurudisha shukrani kwa jamii kwa kutoa misaada ya vitu mbalimbali kwa wahitaji na makundi maalum.

TRA imetoa misaada hiyo Katika Hospitali ya Taifa ya Afya Akili Mirembe na Nyumba ya Matumaini iliyopo Kata ya Miyuji,Jijini hapa ambapo wametoa vitu mbalimbali vikiwemo,Sabuni,Sukari,Unga,Mashuka,Nguo za ndani,viatu,Matunda,Juisi pamoja na Taulo za kike.

Akizungumza wakati akikabidhi misaada hiyo katika Hospitali ya Taifa ya Afya ya Akili,Meneja wa TRA,Mkoa wa Dodoma,Castro John alisema kuwa wamerudisha shukrani hizo katika hospitali hiyo kwasababu wagonjwa wanaotibiwa hospitali hapo ni moja ya wateja wao pindi Afya zao zinapoimalika wanarudi katika shughuli za uzalishaji na akizalisha atalipa kodi kwa maendeleo ya nchi.

“Tunarudisha shukrani hapa kwasababu wagonjwa Mirembe wanafanya juhudi za kuwarudisha katika hali zao za kawaida na wanaotibiwa hapa ni walipa kodi na wakipona wakarudi katika shughuli zao za kila siku za uzalishaji watalipa kodi hivyo tunakona ni vyema kurudisha shukrani hizi,”amesema John.

John amesema kuwa wanajivunia kuwahudumia walipa kodi na wafanyabiahara kwani ni sehemu ya mchakato hivyo wamewaomba walipa kodi nchini kutumia mashine ya EFDs kwani matumizi ya EFDs yanasaidia kuweka kumbukumbu na kupata makadirio ya kodi sahihi kwani wengine wanakuwa wanasema kodi ni kubwa na wakati hawana kumbukumbu hivyo amewasihi kulipa kodi kuhakikisha wanatumia mashine.

Akizungumza wakati wa kupokea msaada huo Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa hospitali hiyo,Dkt.Innocent Mwombeki aliishukuru TRA kwa wa kuwakumbuka nakusema kuwa wanatatambua muunganiko ambao upo katika ukusanyaji mapato kwa vyanzo vya mapato ya nchi kwa maendeleo ya nchi hivyo wamefanya jambo jema kuona kama hospitali hiyo inawahudumia walipa kodi na kurudisha shukrani zao hospitali hapo.

“Lakini pia tuishukuru serikali kwa kutukumbuka katika bajeti tumepewa kipaumbele kwani tulikuwa hatupewi kipaumbele kwenye masula ya afya ya akili,”amesema Mwombeki.

Akipokea misaada hiyo Sista Maria Peter Mwalimu na mlezi katika nyumba ya matumaini ameeleza kuwa katika nyumba hiyo wanahudumia watoto
68 ambapo amesema watoto hao wanawapata kupitia ustawi wa jamii.

Aidha alishukuru kwa msaada huo na kueleza kuwa wanauhuitaji wa vitu vingi kwani wanawahudumia watoto hao toka wadogo,wasoma hadi kufikia umri wa kujitegemea wanawaruhusu kwenda kuendelea na maisha yao sehemu zingine.

“Tunashirikiana na Ustawi wa jamii kuwapata na tunakaa nao katika hatua zote za ukuaji hadi watakapoweza kujitegemea tunawashukuru sana kwani unapotoa umeguswa moyoni ,”amesema Sista Maria.

Maadhimisho hayo yalitanguliwa na matembezi ya shukrani na yatahitimishwa na hafla ya kuwatunuku wafanyabiashara waliofanya vizuri zaidi ili iwe chachu kwa wengine kufanya vizuri.

Awali akizungumza baada ya kutoka kwenye matembezi hayo Mkuu wa Wilaya ya Dodoma Jabir Shekimweri ameipongeza TRA kwa kuendelea kushirikiana vizuri na walipa kodi lakini amesema ni muhimu kuhamasishana watu wote kulipa kodi kwa manufaa ya taifa na kuhakikisha kila mtu anatii sheria bila shuruti.