May 17, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Timu za vijana Simba SC zapata udhamini

Na Mwandishi Wetu, Timesmajira

Klabu ya Simba SC, imeingia mkataba na Kampuni ya MobAd wenye thamani ya Sh. Milioni 500 kudhamini timu za vijana kwa kaulimbiu ya ‘The Future Is Now’.

Simba SC, imeingia Mkataba wa Miaka miwili na Kampuni hiyo wenye thamani ya Sh. 500,000,000 ambapo wanakuwa wadhamini wakuu.

Malengo ya makubaliano hayo ni kuvumbua vipaji, kuvikusanya na kuviendeleaza kwa ajili ya maendeleo ya klabu kwa siku za baadae.

Mtendaji Mkuu wa Klabu ya Simba, Imani Kajula amesema kanuni ya mafanikio ya kila kitu lazima yaanzie mwanzo, hivyo Simba imeona umuhimu wake kurudi kwenye njia zao za zamani.

Kajula amesema sio mara ya kwanza klabu hiyo kuwa na timu za vijana ambazo zimesalisha wachezaji wengi bora ambao mpaka sasa wanatamba na timu mbalimbali za Ligi Kuu ya NBC na zile za Daraja la Kwanza.

“Sisi tunaenda mbele kwa kuleta mfumo wa kutambua vipaji, kuviweka pamoja na kuviendeleaza kutoka sehemu zote nchi nzima. Na tutaweka mfumo mzuri wazi kwa ajili ya kuwapa vijana wenye vipaji kutoka nchi nzima,” amesema Kajula.