March 29, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Tanzania,Ufaransa zakubaliana kushirikiana maeneo ya mkakati

Na David John,TimesMajira Online,Dar es Salaam

SERIKALI ya Tanzania na nchi ya Ufaransa zimekubaliana kushirikiana katika maeneo mbalimbali ya kimkakati kama vile nishati,elimu,kilimo pamoja na miundombinu ambapo Ufaransa imekubali kukarabati Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere ‘Terminal Two’ uliopo mkoani Dar es Salaam.

Waziri wa biashara wa Ufaransa akizungumza na wanahabari mara baada ya kuwasili na ndege ya shirika la ndege nchini ufaransa. Juu ni picha mbalimbali za matukio.

Hayo yamesemwa jijini Dar es Salaam na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki,Balozi Liberata Mulamula (Mb) wakati wa kizungumza na Waziri wa Biashara za Kimataifa na Uwekezaji wa Ufaransa, Franck Riester alipowasili kwa ziara ya kikazi ya siku moja.

Balozi Mulamula amesema Kumekuwa na Miradi mbalimbali ambayo Serikali ya Ufaransa chini ya Shirika lao la Maendeleo wamekuwa siku zote wamekuwa chachu na wamekuwa wakifadhili Miradi katika Sekta mbalimbali hapa nchini hususani katika sekta za Nishati, Elimu, Kilimo na Miundombinu.

Mtakumbuka kuwa Ufaransa ndiyo waliojenga Uwanja wa Ndege wa “Termirnal Two” wa Julius Kambarage Nyerere hivyo wanakuja na mradi wa kukarabati uwanja huo na kuufanya kuwa wa kisasa zaidi.

Amesema Kuwa terminal two imekuwa ikitumika na ndege zinazofanya safari zake za ndani hapa nchini na ,mradi huu ni moja kati ya mradi mkubwa na utakamilika hivi karibuni.

Awali Septemba 15, 2021 Balozi wa Ufaransa hapa nchini Nabil Hajlaouvi amesema Serikali ya Ufaransa kupitia Shirika lake la ndege ‘Fance Airline’ inategemea kuanzisha safari mpya ya ndege kutoka Ufaransa moja kwa moja hadi Zanzibar kuanzia 19 Oktoba 19,2021.

Waziri wa Biashara wa Ufaransa Francka Reister kushoto akiwa na mwenyeji wake Balozi Labereta Mulamula wakizungumzia makubaliano ya kimahusiano.

Wakati huo huo, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula (Mb) ametoa salamu za rambirambi kufuatia kifo cha aliyewahi kuwa waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani, Colin Powell.

“Kwa kweli Serikali ya Tanzania tumeshtushwa sana na kifo chake katika kipindi chake aliendeleza uhusiano wa Marekani na Mataifa mbalimbali, kwa kweli ni masikitiko makubwa tutamkumbuka daima,” amesema Balozi Mulamula.

Naye Waziri Francka Reister wa ufaransa katika mkutano huo amesema wao kama Ufaransa wataendelea kusaidia Serikali ya Tanzania hasa katika seka za kukuza uchumi, miundombinu,na kufanya uwekezaji mbalimbali.

Pia kupitia ziara yake hiyo ya siku moja hapa nchini waziri Francka alifungua duka kubwa vinywaji la kifaransa ambalo lipo uwanja wa ndege wa kimataifa wa Julius kambarage Nyerere teminal three. Akiwa sambamba na mawaziri Kitila Mkumbo, rofesa Makame Mbarawa na mwenyeji waje balozi Mulamula.