May 5, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Tanzania, Norway zasaini mkataba uwekezaji Bil. 7

Na Jackline Martin, TimesMajira Online

Ubalozi wa Norway nchini Tanzania na shirika la umoja wa mataifa la mitaji ya maendeleo (UNCDF) wametia Saini mkataba wa uwekezaji wenye thamani ya shilingi Bilioni
7.4 za kitanzania ili kuwezesha kukabiliana na mabadiliko ya hali ya hewa nchini.

Makubaliano hayo yanalenga kujenga mikakati madhubuti itakayowezesha serikali za mitaa kujenga uwezo, kupanga bajeti, kusimamia na kuripoti maswala yote yanayohusiana na mabadiliko ya tabia nchi.

Akizungumza na waandishi wa Habari Jana Jijini Dar es Salaam Mkuu wa shirika la umoja wa mataifa la mitaji ya maendeleo (UNFDF), Peter Malika amesema makubaliano hayo ni Moja kati ya makubaliano yaliyofanywa na serikali ya Norway pamoja na serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika mashirikiano ya kusimamia mabadiliko ya tabia nchi.

Aidha amesema ushirikiano huo pamoja na ubalozi wa Norway nchini Tanzania ni muendelezo wa miradi mbalimbali ya uwekezaji inayoendelea katika Wilaya ya Chamwino, Kondoa na Mpwapwa ambapo jamii zimeweza kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya hali nchini kupitia suluhisho mbalimbali za kijamii za pamoja na uwekezaji.

“Shirika la UNCDF kupitia mradi wa LOCAL unatoa ruzuku inayotokana na utendaji pamoja na msaada wa kiufundi ili kuweza kusaidia serikali kuweza kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya tabia nchi katika ngazi ya Jamii”

“Tunaendelea kushukuru mashirikiano haya baina ya serikali ya Norway pamoja na serikali ya Tanzania kupitia ofisi ya Makamu wa Rais Idara ya mazingira, Shirika la UNCDF itaendelea kushirikiana na washirika wote wa maendeleo ili kuweza kufanikisha vipaumbele vya kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi”

“Mabadiliko ya tabia nchi yanachangia kwa asilimia kubwa sana katika mafanikio ya Binadamu lakini pia ni chachu katika kufanikisha agenda ya 2030 ya malengo ya maendeleo endelevu maalum katika lengo namba 13” Aliongeza

Kwa upande wake Balozi wa Norway nchini Tanzania Tonne Tinnes amesema serikali ya Norway inathamini mchango wa kuwaleta pamoja washirika mbalimbali wa maendeleo ili kuweza kusaidia kuchukua hatua katika mabadiliko ya Tabia nchi .

“Mabadiliko hayo ni pamoja na shirika la UNCDF yanalenga kujenga uwezo wa Taasisi za serikali za mitaa (TAMISEMI) kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi katika ngazi ya jamii ambayo itawezesha kupanga Mipango madhubuti ya kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi ikiwemo kutenga fedha ili kuweza kuwezesha mikakati hiyo”