April 19, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

TANESCO wayapa elimu wamiliki Migodi, Mashine za kusaga

Na Mwandishi Wetu, TimesMajira Online, Geita

SHIRIKA la Umeme Tanzania (TANESCO) kupitia idara ya masoko, limeendelea na kampeni ya kutoa elimu ya matumizi bora ya umeme kwa wamiliki wa migodi na wamiliki wa mashine za kusaga na kukoboa nafaka Mkoani Geita.

Migodi iliyotembelewa na kikosi kazi hicho cha TANESCO ni pamoja na Migodi ya Geita mjini, Wilaya za Nyanghwale na Bukombe, lakini pia mashine za Posho Mills zilizotembelewa ni za Buseresere Kasamwa, Nyanghwale, Bukombe, Katoro na Geita mjini.

Kwa mujibu wa Mhandisi Ally Koya kutoka kitengo cha masoko Tanesco makao makuu amesema, lengo hasa la kampeni hiyo ni kuwawezesha kufahamu jinsi ya kupunguza gharama ambazo si za lazima kwa kununua vifaa vya kisasa na kuachana na vifaa vilivyochakaa na vya zamani kwani vinatumia umeme mwingi.

Pia wamiliki hao wameelimishwa kuhusu utaraibu wa kufunga mota za kisasa na kuzifanyia huduma mara kwa mara ili mota iendelee kuwa na ufanisi kuelekezwa jinsi ya kufunga ‘power factor’ ili iweze kuwasaidia uendeshaji wa mitambo yaani kVA haitakuwa kubwa.

Afisa Uhusiano na huduma kwa wateja Mkoa wa Geita, akiandika changamoto zinazowakabili wahusika wa moja ya mashine za kusaga walizozitembelea.

“Matumizi bora na sahihi ya umeme ni muhimu kwa usalama kwani umeme ni nzuri kama ukiutumia kwa kuzingatia usalama lakini pia umeme ni moto mara moja, ” amesema Mhandisi huyo.

Hata hivyo, wamiliki wa migodi na mashine walishukuru ujio wa wataalamu hao wa TANESCO kwani umewaongezea uelewa na hivyo kuongeza ufanisi katika eneo la matumizi sahihi ya nishati hiyo ya umeme.