April 24, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Suluhu yaanza kutafutwa Mali

BAMAKO, Wajumbe wa Jumuiya ya Uchumi ya Nchi za Afrika Magharibi (ECOWAS) ambao ni wapatanishi wanatarajiwa kukutana na viongozi wa serikali ya mpito ya Mali ambao wanashikiliwa.

Mazungumzo hayo yanatarajiwa kufanyika leo Mei 26, 2021 ikiwa ni siku mbili baada ya viongozi hao kuondolewa madarakani na jeshi.

Kwa mujibu wa taarifa za awali,Rais Bah Ndaw na Waziri Mkuu Moctar Ouane wanatarajiwa kukutana na ujumbe huo uliowasili mjini Bamako jana.

Kiongozi wa jeshi, Kanali Assimi Goita aliyewaondoa madarakani viongozi hao waliopewa jukumu la kuiongoza serikali ya mpito iliyowekwa mwezi Agosti, mwaka uliopita na kuhakikisha kurejea kwa utawala wa kiraia baada ya mapinduzi amesema, ujumbe wa ECOWAS umeruhusiwa kukutana na kufanya mazungumzo na Ndaw na Ouane.

Naye Kiongozi wa ujumbe huo, rais wa zamani wa Nigeria, Goodluck Jonathan amesema, wameenda Bamako kuwasaidia ndugu zao wa Mali kupata suluhisho la mzozo huo.