May 3, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

STAMICO yatakiwa kuweka mazingira rafiki kwa wachimbaji wadogo

Judith Ferdinand, TimesMajira Online, Mwanza

NAIBU Waziri wa Madini Dkt.Steven Kiruswa amelitaka Shirika la Madini la Taifa(STAMICO) kuendelea kusimamia sekta ya madini kwa kuweka mazingira rafiki kwa wachimbaji wadogo wa madini.

Dkt.Kiruswa amesema hayo Mei 5,2023 wakati alipotembelea banda la STAMICO katika maonesho ya wiki ya madini yanayoendelea katika viwanja vya Rock City Mall mkoani Mwanza.

“STAMICO mnatakiwa kuendelea kusimamia kwa juhudi zaidi sekta ya madini ili kuweza kutatua changamoto za wachimbaji wetu na kuifanya nchi yetu ya Tanzania kuwa kitovu cha biashara ya madini,”.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa STAMICO Dkt. Venance Mwasse amesema shirika hilo kwa kushirikiana na Shirikisho la Wachimbaji wa Madini (FEMATA) wanatoa mafunzo na semina mbali mbali za elimu kuhusu madini kwa wachimbaji wadogo.

Amesema Stamico imekuwa ikisaini mikataba mbalimbali baina yao na kampuni za wadau kwa ajili ya kuweza kuwasaidia wachimbaji wa madini.

Pia amesema shirika lao litaendelea na mipango mbalimbali ikiwemo kusimamia sekta ya uchimbaji madini na kuweka mazingira yatakayoboresha sekta hiyo.

Amesema Shirika lipo katika mipango ya kuendeleza nishati ikiwemo mkaa mbadala wa rafiki briquettes ambao ni nafuu unadumu muda mrefu na unalinda mazingira.

Katika hatua nyingi, Dk Mwasse alipongeza benki ya NMB kwa kuweza kuwakopesha wachimbaji wadogo wa madini fedha ili waweze kufanya shughuli zao huku akisusitiza benki kuachana na dhana ya kuwa wachimbaji wadogo wa madini hawakopesheki.

Aidha amesema shirika litaendelea kukaa pamoja na FEMATA katika kuhakikisha wanafanya utatuzi wa masuala mbalimbali yanayowakabili wachimbaji wadogo hapa nchini.