April 19, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Simba ‘wamkalia kooni’ Mwakalebela

Na Mwandishi Wetu

LICHA ya Makamu Mwenyekiti wa klabu ya Yanga kuuomba radhi uongozi wa klabu ya Simba kufuatia sakata la kiungo wao Mzambia, Clatous Chama, inaonekana vigogo wa Mabingwa hao watetezi wa Ligi Kuu Tanzania Bara (VPL) wamedhamiria kumfikisha kwenye vyombo husika vinavyosimamia soka.

Lakini taarifa za kuhusishwa kuwa mbioni kujiunga na mahasimu wao Yanga msimu ujao , kiungo huyo alikanusha madai hayo huku akidai badi anamkataba wa klabu yake anayoitumikia hivi sasa.

Pia, tayari klabu ya Simba kupitia kwa Afisa Mtendaji mkuu wake, Senzo Mbatha aliweka wazi kuwa, kwenye mpira lazima biashara ifanyike hivyo kama Yanga wanamuhitaji Chama basi wapeleke mezani maombi yao kwani wao kama klabu wapo tayari kuvunja mkataba wa miaka miwili walioingia na mchezaji huyo lakini endapo watakubali kutoa dau la Dola 350,000 ambazo ni zaidi ya milioni 800 za kitanzania.

Juzi kiongozi huyo aliweka wazi kuwa, wanauhakika kuwa mkataba wa kiungo huyo upo mbioni kifika ukingoni hivyo yeye kama kiongozi tayari ameshaanza kufanya naye mazungumzo ili kumshawishi msimu ujao kutua jangwani.

Kauli hiyo iliwatibua viongozi wa klabu ya Simba, ambao jana kupitia kwa Afisa Habari wake, Haji Manara amesema kuwa tayari viongozi wa klabu hiyo wameshaanza mikakati ya kuandika barua kwenda katika Shirikisho la Soka nchini (TFF) kuwashtaki Yanga kwa kosa la kuzungumza na Chama ambae bado ana mkataba wa zaidi ya mwaka mmoja na Simba.

Endapo suala hili litafika kwenye vyombo husika basi huenda ikawa balaa jingine kwa klabu ya Yanga ambao walishawahi kutoswa zaini ya Sh. milioni 50 mwaka 2016 kama fidia ya kukiuka utaratibu wa usajili wa mchezaji Hassan Ramadhani Kessy pamoja na kuitoza faini ya shilingi milioni 3.

Simba ilishinda shauri hilo baada ya kuwasilisha ushahidi wa picha uliomuonesha Kessy yupo na viongozi wa Yanga lakini pamoja na zile zilizomuonesha akisaini mkataba ikiwa bado anamkataba mwingine ya Simba

Manara ame sema kuwa, kitendo kilichofanywa na kiongozi huyo wa klabu kubwa ni kitu cha ajabu sana kwani wao kama klabu walishaweza wazi kuwa mkataba wa Chama unamalizika Julai 2021 hivyo Yanga hawana mamlaka ya kuzungumza na mchezaji huyo.

Amesema, tayari wameshaanza na mchakato wa kuandika barua kwenda TFF ambayo pia itawasilicha CAF na FIFA na moja ya ushahidi watakaotumia ni sauti ya kuongozi huyo alipokuwa anadai ameshaongea na Chama.

Kufuatia tamko la Simba juu ya jambo hilo, Mwakalebela aliamua kuuomba radhi kwa kusababisha sintofahamu hiyo kwani alichokuwa akizungumza ni utani tu kama ambavyo Simba walikuwa wanatania juu ya swala la kiungo wao Tshishimbi.

“Nichukue nafasi hii kuwaomba msamaha Simba na wanachama wa Yanga SC kuhusu kauli yangu juu ya kutaka kumsajili Claotous Chama, nilikuwa nafanya utani kama wao walivyokuwa wanafanya kwa Tshishimbi ila kiukweli mchezaji huyo sijazungumza nae na naahidi jambo hili halitojitokeza tena,” amesema Mwakalebela.

Amesema kuwa, kama kungekuwa na ulazima wa kufanya maongezi na chama, akiwa kama kiongozi wa juu mwenye uweledi katika soka basi angetumia utaratibu kwakuwa anaufahamu.

Mwakalebela pia aliwaomba msamaha viongozi wenzake wa klabu ya Yanga kwani kama ni utani huenda alizidisha kwani baada ya suala la Tshishimbi aliona ni bora nae kuwatania.

“Mbali na kuwaomba radhi klabu ya Simba, lakini pia naomba radhi kwa TFF na klabu yangi ya Yanga kwani huenda labda nilizidisha utani hivyo jambo hili halitajitokeza tena kwangu, kwa sasa naomba tu jambo hili liishe na tuendelee na utani wetu kama ilivyokuwa nyuma,” amesema Mwakalebela.

Lakini licha ya kuomba msamaha huo, inaonekana ni wazi kuwa, klabu ya Simba imedhamiria kumpeleka mbele ya sheria kiongozi huyo.

Manara amesema kuwa, kwa sasa jukumu la kusamehe siyo lake tena kwani tayari ameshalifikisha kwa viongozi wake ambao ndio wataamua nini wanapaswa kufanya.

“Nichokifanya ni kutimiza wajibu wangu wa kuilinda brand kubwa ya kispoti Afrika Mashariki Simba, ambayo sitakubali kwa gharama yoyote ile ichezewe,” aliandika Manara.

Akitolea ufafanuzi wa mkanyangiyo huo, Mwenyekiti wa Chama kinachotetea na kulinda haki za wachezaji nchini (SPUTANZA), Mussa Kisoki alisema kuwa, kama ni kweli kiongozi huyo wa Yanga alifanya mazungumzo na mchezaji huyo ambaye anadaiwa mkataba wake kumalizika 2021 basi atakuwa amekosea.

Amesema, kwa mujibu wa kanuni inapaswa kuanza mazungumzo pale mchezaji anapokuwa amebakisha miezi sita tena kwa kuanza kupeleka barua kwa klabu yake ambayo si lazima ijibiwe, lakini endapo ni kinyume na hapo na wala kutotoa taharifa kwa klabu husika basi ni lazima adhamu itoke kwa klabu husika.