May 17, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Serikali yaipongeza TADB, yaitaka ihamasisha jamii kuwekeza kwenye kilimo

Na Mwandishi Wetu,TimesMajira,Online, Dar

NAIBU Waziri wa Fedha na Mipango, Mhandisi Hamad Masauni amepongeza utendaji kazi wa Benki ya Maendeleo ya Kilimo(TADB) na kuitaka benki hiyo kuendelea kuhamasisha jamii kuwekeza katika sekta ya kilimo, mifugo na uvuvi ili kuchochea ukuaji wa uchumi na maendeleo nchini.

Akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya kufanya kikao na menejimenti alipotembelea makao makuu ya benki hiyo jijini Dar es salaam wiki hii, Mhandisi Masauni amesema kuna haja ya kuelimisha jamii juu ya fursa zilizopo katika kilimo, mifugo na uvuvi kwenye kujiongezea kipato.

“Wananchi wengi wamekuwa wakiwekeza fedha zao kwa mfumo wa bondi za Serikali kwenye benki mbalimbali ambapo faida yake inachukua muda mrefu kulinganisha na kuwekeza kwenye kilimo,” amesema Mhandisi Masauni

Amesema TADB ina kazi kubwa ya kuendelea kutoa elimu kwa wananchi juu ya uwekezaji kwenye mnyororo wa thamani wa kilimo,mifugo na uvuvi ili kuwaaminisha watu kuwa sekta hizi zikitendewa kazi vizuri matokeo yake yatakuwa makubwa katika kuinua uchumi wa wananchi na taifa kwa ujumla.

Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Maendeleo ya Kilimo nchini (TADB) Japhet Justine (kulia) akitoa maelezo juu ya utendaji kazi wa benki yake kwa Naibu Waziri wa Fedha na Mipango Mhandisi Hamad Masauni (kushoto) kwenye kikao cha menejimenti alipotembelea makao makuu ya benki hiyo jijini Dar es Salaam wiki hii. Katikati ni Mwenyekiti wa bodi ya Benki hiyo, Bw.Ishmael Andulile Kasekwa.

“Kauli ya kilimo kinabenkika inatakiwa iwafikie wananchi na kuacha dhana ya kuwekeza fedha kwenye bondi na kuanza kuwekeza kwenye kilimo,mifuko na uvuvi ambapo mavuno yake hupelekea faida kubwa kwa mwekezaji ukilinganisha na uwekezaji wa bondi,” amesema Mhandisi Masauni

Ameongezea kuwa elimu na uhakika wa mikopo pamoja na dhamana katika shughuli za kilimo zitahamasisha katika kuchochea wananchi wengi kujiwekeza katika sekta hizi muhimu ambazo ndio huzalisha malighafi zinazotumika viwandani.

Katika hatua nyingine Mhandisi Masauni ameeleza kuwa amepokea taarifa ya utendaji kazi wa benki hiyo, kwani tangu kuanzishwa kwake mpaka sasa imeweza kutoa zaidi ya sh. bilioni 300 kwa wakulima nchini katika mnyororo wa thamani kwenye sekta ya kilimo, mifugo na uvuvi.

“Serikali itaendelea kutoa ushirikiano kwa TADB kuhakikisha inaendeleza jitihada za kukuza sekta ya kilimo,mifugo na uvuvi ili malighafi ziongezeke na kuhamasisha ujenzi wa viwanda nchini, amesema Mhandisi Masauni

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa TADB, Ishmael Andulile Kasekwa mbali ya kumpongeza Waziri Masauni kwa kuitembelea benki hiyo amemhakikishia kuwa benki hiyo itaendelea kutimiza lengo lake kwa kufuata taratibu na miongozo ya uanzishwaji wake.

“Pamoja na kumpongeza nataka nimhakikishie Wazir Masauni kuwa tutatekeleza vyema lengo la Serikali la kuanzisha benki hii ni kuona benki inashiriki kikamilifu kwenye kuchochea maendeleo ya sekta ya kilimo nchini”. Amesema Kasekwa.

Amesema benki itaendelea kutengeneza mazingira rafiki kwa wakulima ili waweze kunufaika na mikopo nafuu itakayochagiza ufanisi na kuleta tija katika sekta ya kilimo.

“Mimi nichukue fursa hii kuwahimiza wakulima kuendelea kuitumia benki na kuchangamkia fursa tunazozitoa ili kusudi kilimo wanachokifanya kiweze kuwa kilimo chenye tija kitakacho wawezesha kupata kipato kizuri na kuchochea uchumi wa Taifa letu,” amesema Kasekwa.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa TADB Bw. Ishmael Andulile Kasekwa mbali ya kumpongeza Waziri Masauni kwa kuitembelea benki hiyo amemhakikishia kuwa benki hiyo itaendelea kutimiza lengo lake kwa kufuata taratibu na miongozo ya uanzishwaji wake.

“Pamoja na kumpongeza nataka nimhakikishie Wazir Masauni kuwa tutatekeleza vyema lengo la Serikali la kuanzisha benki hii ni kuona benki inashiriki kikamilifu kwenye kuchochea maendeleo ya sekta ya kilimo nchini,” alisema Kasekwa.

Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Maendeleo ya Kilimo nchini(TADB) Japhet Justine (kushoto) akimkaribisha Naibu Waziri wa Fedha na Mipango Mhandisi Hamad Masauni(katikati) alipotembelea makao makuu ya benki hiyo jijini Dar es Salaam wiki hii. Kulia ni Mwenyekiti wa bodi ya TADB, Ishmael Andulile Kasekwa.

Amesema benki itaendelea kutengeneza mazingira rafiki kwa wakulima ili waweze kunufaika na mikopo nafuu itakayochagiza ufanisi na kuleta tija katika sekta ya kilimo.

“Mimi nichukue fursa hii kuwahimiza wakulima kuendelea kuitumia benki na kuchangamkia fursa tunazozitoa ili kusudi kilimo wanachokifanya kiweze kuwa kilimo chenye tija kitakacho wawezesha kupata kipato kizuri na kuchochea uchumi wa Taifa letu”.