May 17, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Serikali: Sekta ya maji inahitaji mabadiliko makubwa

Na Esther Macha,TimesMajira Online,Rungwe

NAIBU Waziri wa Maji Mhandisi Maryprisca Mahundi (MB)amesema kuwa sekta ya maji inahitaji mabadiliko makubwa,mageuzi ili wananchi wafurahie serikali .

Amesema kuwa wanahitaji wananchi wamfurahie Mh Rais mama Samia Suluhu Hassan kwasababu ni mwanamke ambaye ameamua kuhakikisha wanawake wanatua ndoo kichwani na kuona wanawake wanafurahia maisha.

Mhandisi Mahundi amesema hayo jana wakati wa kukabidhi mabomba ya maji tayari kwa utekelezaji kwa ajili ya ukarabati wa miundo mbinu ya mabomba katika Mji wa Tukuyu.

Aidha Mhandisi Mahundi alimpongeza Mbunge wa Rungwe ,Antony Mwantona kwa jitihada za kufuatilia ukarabati wa miundo mbinu ya mabomba Tukuyu Mjini.

Hata hivyo Naibu waziri huyo amebainisha kuwa kama wizara walisema watafia kwenye mitaro ya maji ,matenki tutahakikisha tunatawanyika wote katika maeneo yote ya wananchi.

Aidha Mhandisi Mahundi amesema kuwa wameamua kufanya kazi na watampa heshima mh. Rais Samia kwa dhamana alizowapatia na kwamba matunda hayo ya mabomba ni fedha za awali iliyotangulizwa na wizara ya maji ambapo mradi huo utagharimu Bil.4.5.

NAIBU waziri wa maji Mhandisi Maryprisca Mahundi akizungumza wakati wa kukabidhi mabomba ya maji

“Mh. Mbunge naomba nikuahidi mwishoni mwa mwezi wa mwezi Agosti mwaka huu tutakuletea mil.500 nyingine na kuwa kadri mgao wa fedha hizo unavyokuja wanajitahidi kuwa maji Tukuyu mjini wataishughulikia vizuri”amesema.

Kwa upande wake Meneja Ufundi wa mamlaka ya maji na usafi wa mazingira Mbeya,Mhandisi Barnabas Konga amesema kuwa walipokea fedha kutoka wizara ya maji mil.500 ambapo walinunua mabomba na kusambaza yenye urefu wa kilometa tatu kutoka mto kwenye chanzo cha maji cha mto Masoko.

Naye Mbunge wa Jimbo la Rungwe ,Antony Mwantona ameshukuru wizara ya maji kwa kutoa fedha hizo na kushukuru wizara kwani ilikuwa kilio cha wakazi wa Tukuyu.