May 21, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

SBL, Polisi waanzisha Polisi Jamii Cup 2023

Na Agnes Alcardo, Timesmajira Online, Dar es Salaam

KAMPUNI ya Bia ya Serengeti kupitia kampeni yake ya ‘Inawezekana’ kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi Tanzania,idara ya Usalama Barabarani, imeanzisha mashindano ya mpira wa miguu yajulikanayo kama ‘Polisi Jamii Cup 2023’.

Mashindano hayo, yameanzishwa hivi karibuni, yakiwa na lengo ya kuhamasisha madereva wa vyombo vya moto kutotumia kilevi pindi wanapokuwa barabarani, ikiwa pamoja na kuhamasisha unywaji wa pombe kistaarabu.

Akizungumza katika uzinduzi huo, Mkuu wa Kikosi cha Usalama Barabarani, Kamanda Ramadhani Ng’anzi, amewataka watumiaji wa vyombo vya moto hususani, pikipiki na bajaji kuzingatia sheria za usalama barabarani ili kupunguza ajali za barabarani.

Amesema, suala la kufuata sheria za usalama barabarani, linapaswa kuzingatiwa na watumiaji wote wa vyombo vya moto ili kuepusha ajali .

Ng’anzi amesema, imekuwa ni kawaida kwa madereva wa pikipiki (bodaboda), kujiona wapo juu ya sheria na kuvunja sheria za usalama barabarani kwa kusudi, jambo ambalo vyombo husika vya usalama havina budi kuchukua hatua.

Aidha, kwa upande wake, Mkurugenzi wa Masoko na Ubunifu wa Kampuni ya bia ya Serengeti (SBL), Anitha Msangi, amesema wataendelea na utaratibu wa kuwapongeza watumishi wanaofanya vizuri ili kujenga motisha kwa watu kufanya kazi kwa bidii.

Nae Meneja Mawasiliano na Uendelevu wa SBL, Rispa Hatibu, alithibitisha imani ya kampuni hiyo ya kuhamasisha kunywa kwa uwajibikaji ni jukumu la kibinafsi, akisema, “SBL inaamini kwa dhati kwamba kunywa kwa uwajibikaji huanzia kwa mtu.

“Kampeni ya INAWEZEKANA inalenga kukuza na kuhamasisha tabia ya unywaji pombe kwa kuwajibika na usalama barabarani katika jamii yetu,” alisema.

SBL inajivunia kuungana na polisi wa Trafiki wa Tanzania kukuza unywaji pombe wa kistaarabu na usalama barabarani. Ushirikiano huu umepangwa kushirikisha waendesha pikipiki wenye shauku katika ngazi zote za mashindano, kuanzia ngazi ya kata hadi ya Taifa.