May 3, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Rais Samia aunda baraza la Kilimo,Chakula

Na Penina Malundo, timesmajira

RAIS Dkt. Samia Suluhu Hassan ameunda baraza la kumshauri Rais linalohusu utekelezaji wa masuala ya Kilimo na Chakula (Presidential Food and Agriculture Delivery Council) na kumteua Waziri Mkuu Mstaafu,Mizengo  Pinda kuwa Mwenyekiti baraza hilo.

Taarifa iliyotolewa leo na Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais Ikulu,Zuhura Yunus  alisema  wajumbe wengine walioteuliwa na Rais Samia  ni pamoja na Mkurugenzi Mtendaji wa SAGCOT,Geoffrey Kirenga  na Katibu Mkuu Mstaafu,Andrew Masawe  kuwa wajumbe wa baraza hilo.

Pia amewateua wajumbe wa Sekretarieti ya Baraza hilo ni pamoja na Katibu Mkuu Mstaafu na Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo(SUA),Dkt. Florence Turuka,Mkurugenzi Mtendaji wa Tanzania Herticulture Association (TAHA),Dkt.Jacqueline Mkindi  na Mwenyekiti wa Tanzania Organic Agricultural Movement (TOAM),Dkt. Mwatima Juma.

Yunus amesema katika kutekeleza azimio la Viongozi wa nchi za Afrika kupitia mkutano wa utoshelevu na Ustahimilivu wa Chakula  uliofanyika Dakar ,Senegal Januari 25 hadi 27 ,2023 waliazimia kila nchi kuunda Mabaraza ya kusimamia utekelezaji wa mikakati ya kukuza kilimo na kuongeza uzalishaji wa chakula ili kufikia azma hiyo.

Amesema baraza hilo linatarajiwa kuzinduliwa rasmi Machi 17,mwaka huu Ikulu Dar es Salaam.