May 18, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Lazaro Mambosasa,

Polisi yazuia mikusanyiko kwenye fukwe Pasaka

Na Francis Peter

JESHI la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam limepiga marufuku
mikusanyoko kwenye fukwe, katika kumbi za starehe na disko wakati wa
Sikukuu ya Pasaka kwa lengo la kukabiliana na maambukizi ya ugonjwa wa
Corona.

Uamuzi huo umetangazwa jijini Dar es Salaam jana na Kamanda wa Polisi
Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Lazaro Mambosasa, wakati akizungumza na
waandishi wa habari.

Alisema Polisi wamejipanga kuimarisha ulinzi wakati wa Sikukuu zote za
Pasaka nchini. Alisema Sikukuu hizo zinaheshimika na kwamba
watahakikisha wanalinda amani kwa raia wote.

Kuhusu kuwepo kwa ugonjwa wa Corona, alishauri familia kusherehekea
sikukuu hiyo pamoja isipokuwa mikusanyiko ya kwenda kwenye fukwe,
kumbi mbalimbali za starehe ikiwemo disko haitaruhusiwa.

“Kutokana na hofu ya maambukizi ya kusambaa kwa virusi vya
Corona, Jeshi la Polisi tumekataza mikusanyiko hiyo,” alisema.

Wakati huo huo, Kamanda Mambosasa alisema Polisi Kanda hiyo Maalum ya
Dar es Salaam wanamshikilia Mohamed Kassim (47) mkazi wa Mbagala kwa
tuhuma za kumiliki silaha kinyume na sheria.