April 16, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Ngumi za ridhaa kuanza kutimua vumbi Julai 14

Na Mwandishi Wetu, Timesmajira Online

MASHINDANO ya wazi ya kugombea ubingwa wa taifa ngumi za ridhaa, yanatarajiwa kuanza kutimua vumbi Julai 14 hadi 18, kwenye uwanja wa ndani wa taifa (indoor), jijini Dar es salaam.

Mashindano hayo yatahusisha wachezaji kutoka mikoa ya Dar es salaam, Morogoro, Mwanza, Iringa, Tanga, Kagera na Singida ambao hadi sasa wamethibitisha ushiriki wao.

Akizungumzia hilo, Katibu mkuu wa shirikisho la ngumi za wazi Tanzania (OBFT), Lukelo Wililo amesema lengo la mashindano hayo ni kuwapa nafasi mabondia wa ngumi za ridhaa ambao hawajawahi kufika ama kuonekana katika medani za kitaifa.

“Kimsingi mashindano haya huibua vipaji vipya vya ngumi, ambapo kumekuwa na mabondia kadha wa kadha wanaofanya vema kwenye ngumi za kulipwa ambao ni chimbuko la mashindano hayo.

“Mfano, Selemani Kidunda, Rashid Matumla, Ismail Galiatano, ni baadhi ya mabondia waliopitia katika mashindano hayo, ambao walifanya na wanafanya vyema kwenye ngumi za kulipwa,” amesema Wililo.