April 26, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Mkurugenzi wa Taasisi Mwamvuli ya kilimo hai nchini Bakari Mongo akizungunza mbele ya waandishi wa habari hawapo pichani.

Nchi tano kushiriki kongamano la kimataifa la kilimo hai nchini

Na David John,TimesMajira,Online

NCHI  tano za Afrika na Ulaya zitashiriki kongamano la kimataifa la Kilimo hai,linalotarajia kufanyika Novemba 23,2020 jijini Dar es Salaam litakalojadili ‘Uhuru wa mbegu na utunzaji wa Bioanuai’.

Kongamano hilo limeandaliwa na Taasisi mwamvuli wa Kilimo hai Tanzania (TOAM) na Mtandao wa Mashirika yasiyo ya kiserikali na sekta binafsi ,inayojishughulisha na utunzaji bioanuai ya Kilimo Tanzania (TABIO)

Akizungumza leo na waandishi wa habari,Mkurugenzi wa TOAM, Bakari Mongo, amesema kuwa kongamano hilo litawaleta pamoja washiriki mbalimbali kutoka Serikalini, vyuo vikuu pamoja na wadau wengine.

Amesema kuwa lengo la kuwaleta pamoja ni mwendelezo wa majadiliano na kujengeana uwelewa hususani kuhusu matumizi ya mbegu za vinasaba na faida na athari zake.

“Mazao yaliyobadilishwa vinasaba yamekuwa yakipigiwa chapuo kama suluhishi la changamoto katika Kilimo hapa Tanzania, wakati ikielezwa kuna faida kwenye mbegu hizo lakini pia kuna athari za kijamii na kiuchumi zinazoambatana na matumizi yake ambapo ambazo idadi kubwa ya watu hawazifahamu,” amesema Mongo.

Amesema kongamano hilo litajadili athari hizo na umuhimu wa usalama wa mbegu kwa ajili ya kizazi cha sasa na cha baadae.

Aidha,  Mratibu wa TABIO, Abdallah Mkindi amesema kuwa mbegu ni kiunganishi cha kwanza katika mnyororo wa chakula na hivyo ni jukumu la kila mmoja kuzilinda na kuzirithisha kwa vizazi vijavyo.

Amesema serikali kwa upande wake nao watakauwepo kwenye kongamano hilo kusikia majadiliano kutoka kwa wakulima juu ya usalama wa mbegu.

Kongamano hilo la siku moja litafanyika kwenye ukumbi mpya wa maktaba ya chuo kikuu cha Dar es Salaam.