April 23, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Muhimbili yawatenganisha pacha walioungana

Na.Mwandishi wetu,timesmajira,Online

Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Samia Suluhu Hassan imedhamiria kuboresha ubora wa huduma ya afya hususani kwenye huduma za Ubingwa na Ubingwa Bobezi.

Katika kudhihirisha hilo Julai Mosi,Hospitali ya Taifa Muhimbili ilifanya upasuaji mkubwa na wa mafanikio wa kuwatenganisha watoto pacha (Rehema na Neema) waliozaliwa wakiwa wameungana sehemu ya kifua,tumbo na Ini kwa maana kila mtoto alikua na Ini lake na upasuaji huo ulichukua saa 7 na uliwajumuisha watalaamu zaidi ya 31 wakiwemo madaktari upasuaji watoto, wauguzi,wataalamu wa usingizi na ganzi kwa watoto,daktari upasuaji mifupa watoto ambapo pia walishirikiana na wenzao kutoka Hospitali ya Chuo Kikuu cha King Hamad nchini Bahrain.

Sekta ya afya nchini imejiwekea vipaumbele ambavyo Serikali ya Rais Samia Suluhu Hassan ingependa kuviona vinatekelezwa na kipaumbele kikubwa ni ubora wa huduma za afya katika kuokoa maisha ya wananchi wake.

Serikali ya Awamu ya Sita katika kuhakikisha kuwa huduma za afya nchini zinaboreshwa katika kipindi cha mwaka mmoja imewekeza kwa kuboresha miundombinu ya kutolea huduma, kusomesha watalaamu, ununuzi wa dawa, vifaa na vifaa tiba pamoja na huduma za kibingwa na ubingwa bobezi kwenye hospitali zote nchini zikiwemo hospitali za Wilaya,Mikoa,Kanda,Maalumu na zile za Taifa.