May 14, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Msama atoa wito kwa wasanii nchini mikopo ya serikali

Na Jackline Martin, TimesMajira Online

Wasanii wameshauriwa kutumia mikopo yao waliyopewa na Rais Dkt Samia Suluhu Hasan waitumie katika mambo yale yaliyokusudiwa ili iweze kuwanufaisha wenyewe katika kuikuza tasnia ya sanaa nchni.

Mikopo hiyo ikiwa ni ya awamu ya pili kwa wasanii, serikali ilitoa shilingi Milioni 850 kwa wasanii 40 nchini, ambayo wasanii waliiomba kupitia wizara ya utamaduni, sanaa na michezo.

Wito huo umetolewa leo jijini Dar es salaam na mkurugenzi wa kampuni ya Msama promotions inayoandaa matamasha mbalimbali ya injili nchini, Alex Msama wakati akizungumza na waandishi wa habari, na kusema kuwa Lengo la mikopo hiyo ni kuwasaidia wasanii wote, iwainue na waikuze sanaa yao.

“Kupitia mikopo hiyo, mfanyie mambo ya msingi, mtunge nyimbo nzuri na mambo mengine ya maendeleo ili mjiinue kiuchumi”

“Tunamshukuru Rais Dkt Samia Suluhu Hassan kwani ana upendo wa hali ya juu, mwenye hofu ya Mungu, na mwenye upendo wa dhati kwa watanzania hasa kwa kuwakumbuka wasanii wote wa Tanzania kwa kuwapa mikopo” Amesema Msama.

Aidha Msama amesema endapo mikopo hiyo wakiitumia vizuri itasaidia na wengine kuweza kukopeshwa ili kukuza uchumi wa Taifa kwa ujumla.

Msama alimshukuru, Waziri wa Habari, Utamaduni na Michezo, Mohamed Mchengerwa na Katibu Mkuu wa wizara hiyo Dkt. Hassan Abas kwa kufanya kazi nzuri wanayoifanya kwa upande wa tasnia ya sanaa ambapo amewataka wasanii kuunga mkono juhudi hizo za serikali.

Mratibu wa tamasha hilo la injili, Emmanuel Mabisa amesema Maandalizi ya Tamasha la pasaka litakalofanyika Aprili 4 mwaka huu Jijini Dar es Salaam yapo vizuri, ambapo kwa wiki ijayo wataanza kutangaza majina ya waimbaji watakaoimba katika tamasha hilo kutoka ndani na nje ya nchi.