April 20, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Miundombinu maeneo ya kihistoria kuendelea kuhimarishwa Zanzibar

Na Haji Mtumwa, TimesMajira Online, Zanzibar

WAZIRI wa Utalii na Mambo ya Kale Zanzibar, Simai Mohamed Said amesema kuwa, ataendelea kuimarisha miundombinu katika maeneo ya kihistoria pamoja na kutangaza vivutio vya utalii ili kuhakikisha idadi ya wageni inaongezeka zaidi na kukuza uchumi wa nchi.

Kauli hiyo ameitoa katika kikao cha majumuisho na kutathimini utekelezaji wa majukumu ya wizara hiyo mbele ya Kamati ya Biashara Kilimo na Utaliii ya Baraza la Wawakilishi ambapo kikao kazi hicho kimefanyika ofisini kwake Kikwajuni, Mjini Unguja.

Waziri Simai amewaeleza wajumbe wa kamati hiyo kuwa moja ya vipaumbele vyake ni kuhakikisha anaimarisha miondombinu katika maeneo ya kihistoria pamoja na kuongeza nguvu ya kutangaza vivutio vya utalii vilivyopo nchini.

“Nitahakikisha naendelea  kuimarisha miundombinu katika maeneo ya kihistoria pamoja vivutio vya utaliii ili kuhakikisha idadi ya wageni inaongezea zaidi na kuinua pato la nchi,” alisema.

Aidha Waziri Simai alisema kuwa wizara itahakikisha inaendeleza mashirikiano na wadau mbalimbali katika kuimarisha ulinzi na usalama kwa watalii.

Aliongeza kuwa, wizara imeweka mpango mkakati madhbuti wa kuimarisha mji katika hali ya usafi nakuwavutia wageni wengi zaidi.

Katika maelezo yake Waziri Simai alisema kuwa, wizara itaandaa mpango madhubuti kuhakikisha wageni wote wa nalipa kodi stahili wanapoingia nchini pamoja na kurahisishiwa njia ya huduma za kifedha ili kurahisisha huduma hizo.

Kwa upande wake Katibu Mkuu wa Wizara ya Utaliii na Mambo ya Kale,  Fatma Mabrouk Khamis amewahakikishia wajumbe wa Kamati ya Biashara Kilimo na Utaliii wa Baraza la Wawakilishi  Zanzibar, kupatiwa mafunzo kuhusiana na mambo ya kale ili kuweza kuishauri wizara kikamilifu na kuleta ufanisi.

Nae  Mwenyekiti wa Kamati hiyo ambae pia ni Mwakilishi wa Jimbo la Fuoni,  Yussuf Khamis Idd ameupongeza uongozi na watendaji wa Wizara ya Utaliii na Mambo ya Kale kwa ripoti nzuri Iliyowasilishwa na kuwaomba kuendelea kushirikiana katika kutekeleza majukumu ya kikazi sambamba na kuzifanyia kazi ripoti za mkaguzi wa ndani kwa lengo la kuzipatia ufunguzi kasoro za kiutekezaji zinazojitokea.