April 26, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

TEHAMA kutumika kupima utendaji kazi serikalini

Na Mwandishi Wetu, TimesMajira Online

IMEELEZWA kuwa utekelezaji wa maagizo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan ya kuitumia mifumo ya TEHAMA katika kupima utendaji serikalini ili kuimarisha uwajibikaji na utoaji Huduma bora.

Katibu wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikali za Mitaa Tanzania (TALGWU), Rashid Mtima (Kushoto) akifuatilia Mkutano na Viongozi wa Vyama vya Wafanyakazi kuhusu mtazamo wa serikali ya Awamu ya sita katika Uimarishaji wa Utumishi wa Umma unaowajibika kwa hiari na Matumizi ya mifumo ya TEHAMA katika utendaji na utoaji Huduma bora katika Utumishi wa Umma, leo jijini Dodoma

Wakiongea mapama leo jijini Dodoma, Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira, Vijana na Wenye Ulemavu), Joyce Ndalichako pamoja na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi na Utawala Bora, Jenista Mhagama wakati wa mkutano na viongozi wa vyama vya wafanyakazi kuhusu mtazamo wa serikali ya awamu ya sita katika uimarishaji wa utumishi wa umma unaowajibika kwa hiari na matumizi ya mifumo ya TEHAMA katika utendaji na utoaji huduma bora, wamefafanua kuwa serikali inaendelea kufanya maboresho ya kisekta mtambuka ya kujenga mifumo ya TEHAMA.

Ndalichako amefafanua kuwa pamoja na juhudi za serikali za kupima utendaji kazi serikalini Rais amelekeza ushirikishwaji wa Vyama vya Wafanyakazi amewataka Vioongozi wa Vyama vya Wafanyakazi kuendelea kuwa daraja kati ya waajiri na Wafanyakazi kwa kuchochea na kuhimiza utamaduni kwa Wafanyakazi kudai haki na kutimiza wajibu wao.

Ameongeza kuwa Ofisi ya Waziri Mkuu- Kazi, Ajira, Vijana na Wenye Ulemavu imeendelea kutekeleza maagizo ya Mhe, Rais kwa kukamilisha Mfumo wa Kielektroniki wa utoaji wa Vibali vya Kazi kwa raia wa kigeni. Mfumo huo umepunguza muda wa kushughulikia maombi ya vibali vya kazi kutoka siku za kazi 14 hadi siku 7. Aidha, Mfumo huo umeimarisha uwazi na uwajibikaji.

Kwa upande wake Mhagama amebainisha kuwa Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi na Utawala Bora amefafanua kuwa Ofisi hiyo imetekeleza maagizo ya Rais kwa kujenga na kufanya maboresho katika mifumo ya Usimamizi wa Utendaji Kazi kwa Watumishi wa Umma (PEPMIS), Usimamizi wa Utendaji kazi katika ngazi ya Taasisi (PIPMIS).

Rais wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi (TUCTA) Tumaini Nyamhokya (wa kwanza kulia ) akifuatilia Mkutano na Viongozi wa Vyama vya Wafanyakazi kuhusu mtazamo wa serikali ya Awamu ya sita katika Uimarishaji wa Utumishi wa Umma unaowajibika kwa hiari na Matumizi ya mifumo ya TEHAMA katika utendaji na utoaji Huduma bora katika Utumishi wa Umma, leo jijini Dodoma.

Mhagama amebainisha kuwa mifumo mingine ambayo imetekelezwa na Ofisi hiyo kuwa ni; Mfumo wa e-mrejesho, Mfumo maalum wa Tathmini ya hali ya Rasilimaliwatu, Mfumo wa Huduma Mtandao kwa Watumishi (Watumishi Portal) pamoja na mfumo wa SEMA NA WAZIRI.

Ameongeza, Mhagama amesisitiza kuwa utekelezaji wa maagizo hayo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan ni kuhakikisha Dira na maono  yake yanakamilika ambapo anapenda kuwa na Utumishi wa Umma unaofanya kazi kwa: Uadilifu; Uwajibikaji; Bidii na Weledi; Haki na Uzalendo wa Kitaifa.

Amewataka Viongozi wa Wafanyakazi pamoja na kusimamia haki na maslahi ya Watumishi wa Umma kuhakikisha wanawasimamia Watumishi wa Umma ilikuhakikisha wanachapa kazikwa utalaam, ubunifu, weledi wa hali ya juu na kwa kuzingatia maadili ya utendaji katika Utumishi wa Umma ili kufikia Dira, Maono na Azma ya Kiongozi Mkuu wa Nchi yetu.

Katika hatua nyingine, Viongozi wa Vyama vya Wafanyakazi wamewapongeza Mawaziri hao na kuipongeza serikali ya Awamu ya sita inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan,  kwa kujenga mifumo mipya ya TEHAMA inayoimarisha Utumishi wa Umma wa uwajibikaji wa hiari, hali hiyo imeonesha dhamira ya dhati ya serikali ya  kuwajali wafanyakazi nchini.