March 29, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Mfumo wa tathimini ya hali ya watumishi wazinduliwa

Na Joyce Kasiki, TimesMajira Online, Dodoma

WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Jenista Mhagama amezindua Mfumo wa Kielektroniki wa tathimini ya hali ya watumishi katika Utumishi wa Umma ambao umelenga kuweka msawazisho wa watumishi wa Umma katika Utumishi wa Umma kwa lengo la kuongeza tija katika utendaji kazi.

Aidha Mhagama amewaagiza waajiri wote wawasimamie Wakurugenzi au Wakuu wa Idara/Sehemu  zinazosimamia Rasilimaliwatu katika taasisi zao ili wakamilishe zoezi hilo kabla au ifikapo tarehe 31 Machi, 2022.

Alisema,Taasisi  ambazo hazitakamilisha zoezi hilo kwa muda uliowekwa , zitakuwa zimekiuka maelekezo ya Serikali na hatua stahiki zitachuliwa dhidi yao.

Ni imani yangu kuwa, Wakuu wa Taasisi za Umma na watumishi watazingatia maelekezo niliyotoa na yale  ambayo yamekuwa yakitolewa  kwa ajili ya kulifanya zoezi hili liwe na tija…,na kwa kufanya hivyo tutaweza kufikia azma ya Samia Suluhu Hassan Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wa Awamu ya Sita kuwa na Utumishi wa Umma wenye uwiano wa watumishi unaouzingatia mahitaji na ujuzi stahiki katika maeneo husika.  “

Akizungumza jana na waandishi wa habari ofisini kwake Mtumba jijini Dodoma muda mfupi kabla ya kuzindua mfumo huo ,Mhagama alisema madhumuni ya Mfumo huo ni kuwa na Utumishi wa Umma wenye uwiano wa watumishi unaouzingatia mahitaji na ujuzi stahiki katika maeneo husika.

Wafanyakazi Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma wakimsikiliza Waziri wa Ofisi hiyo Jenista Mhagama wakati wa uzinduzi wa Mfumo wa Kielektroniki wa tathimini ya hali ya watumishi katika Utumishi wa Umma

Alisema licha ya kwamba zoezi hilo kuanza tangu mwezi Januari mwaka huu na lilitakiwa likamilike katikati ya mwezi Februari mwaka huu  lakini zoezi linaonesha bado Wizara na Taasisi nyingi hazijakamilisha zoezi hili muhimu.

“Kwa taarifa tulizonazo mpaka leo kati ya Wizara na Taasisi 427 zilizo kwenye Mfumo wa HCMIS, zote zimeshaanza kutumia Mfumo na zipo katika hatua mbalimbali za utekelezaji wa zoezi hili na zipo kati ya asilimia 13 hadi 97. “alisema

Aidha, alisema,taasisi 41 kati ya taasisi 70 zilizo nje ya Mfumo wa HCMIS zimeshawasilisha taarifa zao na sasa wataalam wanachakata taarifa hizo kwa ajili ya kuziweka kwenye Mfumo.

 Hata hivyo Mhagama alisema,bado kuna Wizara na Taasisi nyingi hazijatekeleza maelekezo ya Serikali ipasavyo huku akiwataka  viongozi wa taasisi wawajibike ipasavyo ili  kufikia lengo la zoezi hilo muhimu litakaloimarisha usimamizi wa Rasilimaliwatu.

Aidha Waziri huyo alisema,taarifa za kwenyeMfumo huo zimebainisha kuwa zipo Taasisi zilizofanya vizuri na ambazo hazijafanya vizuri katika kuingiza taarifa kwenye Mfumo.

Amezitaja Taasisi 10 bora zilizofanya vizuri katika kuingiza taarifa za watumishi wao kwenye mfumo huo kuwa ni  pamoja na Shule ya Sheria Tanzania (97%), Tume ya Ushindani (97%), Chuo cha Ardhi Morogoro (97%), Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala (96%) na  Ofisi ya Rais Kumbukumbu na Nyaraka za Taifa (95%).

Ofisi nyingine ni Sekretarieti ya Mkoa wa Iringa (95%), Wakala ya Mafunzo ya Mifugo (95%), Mamlaka ya Serikali Mtandao (95%),Taasisi ya Utafiti wa Wanyama Pori (95%) na Wakala ya Mafunzo ya Menejimenti ya Elimu (94%).

Vilevile alisema  Mfumo huo pia umebainisha Taasisi takribani 94 ambazo hazijafanya vizuri katika kuingiza taarifa kwenye Mfumo kwa sababu bado zipo chini ya asilimia 50 ya utekelezaji wa zoezi hilo.

“Kwa mfano, wenzetu wa Mamlaka za Serikali za Mitaa takribani Halmashauri 39 na Mamlaka nyingi za Maji hawajafanya vizuri kwenye zoezi hili.”

 “Katikakutekeleza majukumu iliyopangiwa, Ofisi yangu itahakikisha inazingatia Dira ya Taifa ya Maendeleo ya mwaka 2030; Ilani ya Uchaguzi wa Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2020 – 2025; Mpango wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka Mitano wa Awamu ya Tatu 2021/22 – 2025/26,

“Pamoja na maono ya Rais wa Serikali ya Awamu ya Sita na Amiri Jeshi Mkuu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kuhusu Utumishi wa Umma wa kidijtali na unaofanya kazi kwa uadilifu, kwa bidii, unaotenda haki, unaowajibika kwa hiari na unaozingatia uzalendo wa kitaifa.Alisema Mhagama na kuongeza kuwa

“Ni jukumu letu sisi Viongozi na Watumishi wote wa Ummakuchapa kazi kwa utalaamu, ubunifu na weledi wa hali ya juu ili kuhakikisha kuwa Dira ya Maendeleo ya Taifa na maono na azma ya Kiongozi Mkuu wa Nchi yetu yanatimia.”

Ametumia firsa hiyo kuwataka watumishi wote kuutunza , kuusimamia na kuulinda Mfumo huu ili uweze kufanya kazi iliyokusudiwa ipasavyo.

Aidha Mhagama alibainsiha kuwa Mfumo huo pia umlenga kkuwezesha kukusanya, kuchakata na kuchambua taarifa za Watumishi kwa njia ya kisayansi ili kubaini mahitaji halisi ya Watumishi katika Wizara na Taasisi za Umma.

“Zoezi hili litatusaidia katika kutathmini hali halisi ya Watumishi waliopo na wanaohitajika katika taasisi zote za umma ili kuweza kuwapanga kwa kuzingatia mahitaji halisi ya kila taasisi.”

Alisema kwa kufanya hivyo, Serikali itakuwa na taarifa na takwimu sahihi kuhusu watumishi waliopo, mahitaji ya watumishi wanaohitajika katika kutekeleza majukumu ya kuwahudumia wananchi.

Kwa mujibu wa Mhagama, matarajio ya zoezi hilo ni kuweka msawazisho wa Watumishi wa Umma katika taasisi za Umma huku akisema,kwa tathmini iliyopo inabainisha kuwa utoshelevu wa mahitaji ya watumishi kwa taasisi za Umma upo kati ya asilimia 52 hadi 90.