May 14, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

MCT yazungumzia sheria za vyombo vya habari

Na Penina Malundo,Timesmajira Online.

KATIBU Mtendaji wa Baraza la Habari Tanzania (MCT), Kajubi Mukajanga amesema bila kushughulikia sheria za vyombo vya habari nchini, tatizo la kufungia kwa vyombo hivyo halitaweza kuisha badala yake litaendelea.

Ameyasema hayo juzi mkoani Morogoro wakati wa ufunguzi wa mafunzo kwa vyombo vya Habari vya Mtandao (Media Online), yenye lengo la kuwajengea uwezo wa namna ya kufanya kazi zao kwa weledi kwa kufuata misingi ya sheria ya uandishi wa habari.

Mukajanga amesema, kutokufutwa kwa sheria zinazolalamikiwa na zilizokandamizi kwa vyombo vya habari, tatizo kufungia halitaweza kuisha.

Amesema agizo la Rais, Samia Suluhu Hassan la kuvifungulia vyombo vya habari vilivyofungiwa kutokana na sababu mbalimbali, jambo hilo bado lina mjadala sababu wengine walisikia Rais Samia ametamka vyombo vya habari.

“Wasaidizi wake wamesema agizo hilo, lilihusu vyombo ya habari vya mtandaoni hivyo kwa sababu ofisi yake haijatoa kauli juu ya taarifa ya wasaidizi wake hao, agizo la kufunguliwa kaw vyombo vya habari bila shaka hilo ndiyo sahihi.

“Tunadhani bila kushughulikia sheria zinazoongoza, zinazosimamia na kudhibiti kazi zetu, tatizo halitaweza kuondoka, inaweza kuwa kwa nia njema Kiongozi anaweza akaamua kama hivyo mfungulieni fulani, lakini kama sheria ipo maana yake kesho anaweza kupata tatizo mtu mwingine, au yuleyule aliyefunguliwa akapata tatizo kutokana na sheria zile zile,” amesema.

Kwa upande wake Mratibu wa Taifa wa Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu Tanzania (THRDC),
Onesmo Ole Ngurumwa amesema waandishi hao wanapaswa kufanya kazi zao vizuri za kuhabarisha umma, huku akisema mtu anaposema matumizi ya mtandao anazungumzia uhuru wa kujieleza.

Amesema ni muhimu vyombo vya habari vya mtandao, vikasimama vizuri na kuwa wanataaluma wazuri ambao watazingatia misingi, sheria, kanuni, taratibu za taaluma ya uandishi wa habari katika utaekelezaji wa majukumu yao.

Naye Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri Tanzania, Deodatus Balile amesema mtandao wa THRDC unawezesha vyombo vya habari vya mtandao kuwa uchumi unaotengamaa, kwani vingi havina mipango ya biashara huku akiwasisitiza waandishi wa habari kuwa na hali ya kujijali.