April 16, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Mbunge wa Bahi Kenneth Nollo

Mbunge Nollo kuzindua zahanati tano kijiji cha Nguji

Na Joyce Kasiki,TimesMajira,Online

MBUNGE wa Bahi Kenneth Nollo (CCM) anatarajia kuzindua ujenzi wa zahanati tano katika kijiji cha Nguji ambazo zinajengwa ili kusogeza huduma za Afya kuwa karibu na wananchi na kupunguza vifo vinavyoweza kutokea kwa kukosa huduma za Afya.

Akizungumza na gazeti hili Bungeni jijini Dodoma Nollo amesema katika Jimbo hilo wana upungufu wa zahanati 11 na kwamba wanahitaji angalau zahanati chache za kuanzia ili wananchi wapate huduma hizo bila usumbufu na kuondoka changamoto zinazoweza kujitokeza ikiwemo za vifo.

“Katika Jimbo la Bahi tunahitaji zahanati 11 hadi 12 ,kwa nafasi hii niliyoipata nitawahamasisha wananchi tushirikiane kuzijenga ambapo wao watachangia nguvu kazi .” amesema Nollo  na kuongeza

“Wiki ijayo nitazindua Ujenzi wa zahanati tano katika kijiji cha Nguji ,sisi tutaanza na tulichonacho na pale tutakapoishia tutaiomba Serikali itupokee katika hatua zinazofuata ,maana huwezi kupata lifti kama umekaa nyumbani  kwahiyo tukifika sehemu tutaomba msaada kwa serikali.” Amesema mbunge huyo

Aidha mbunge huyo amesema pia kipaumbele kingine atakachoanza nacho ni kuchimba visima ili kuwawezesha wananchi wa Jimbo hilo kufanya kilimo cha umwagiliaji na hivyo kuwafanya wananchi kujishugjulisha na shughuli za kiuchumi wakati wote.

“Kama tunavyojua Dodoma ni kame tofauti na maeneo mengine ,hali hiyo pia inasababisha changamoto ya maji safi na maji kwa ajili ya kilimo.” Amesema

Amesemakutokana na changamoto huyo atachimba visima ili kuboresha upatikanaji wa maji ambao utawawezesha wananchi kufanya kilimo cha umwagiliaji.