May 4, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Mbowe afunguka mazito tuhuma za kulamba asali

Na Mwandishi wetu, Timesmajira Online Mwanza

MWENYEKITI wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Freeman Mbowe akiwa Mwanza kwenye Mkutano wa kwanza wa hadhara wa Chama hicho toka Rais Samia aliporuhusu mikutano ya Vyama vya siasa amesema hajalamba asali kama baadhi ya Watu wanavyodai huku akisema amepoteza Mabilioni ya fedha kukipigania Chama hicho na hawezi kuwasiliti Wanachama kisa fedha au mali.

“Yaani mnaanza kusema eti Mbowe kalamba asali, hivi mnajua Mbowe nimepoteza Bilioni ngapi kwakuwa Mwana CHADEMA?, mnakubali kutunza propaganda za kitoto kwamba eti Mbowe kalamba asali hataki Katiba Mpya, hataki Tume huru so what?, upande wa pili naweza kuelewa vilevile hisia za Viongozi na Wanachama wa CHADEMA kwa maumivu ambayo tumeyapitia kwa muda mrefu”

“Kwahiyo wakitoka Wanachama wa CHADEMA wakahofu maamuzi ya Mwenyekiti binafsi nawaunga mkono naelewa kwasababu tumeumizwa sana, ni asilimi 2 tu ya Wanachama wa CHADEMA wanaiamini CCM lakini Mimi niliwaamini kwa kiwango fulani niliokuwa nazungumza nao”

“Tulipoanza mazungumzo tulikubalina misingi ikiwemo usiri, Wanachama wa CHADEMA wakiwemo Viongozi wangu Wakuu wakasema ‘Mbowe anafanya usiri hatuambii, yupo Ikulu kila siku, hii Mi-CCM sio ya kuiamini, kalamba asali’, yaani kama kuna kitu kimewahi kuniumiza ni kuwepo kwa Mtu anayeweza kuamini kwamba eti Mimi naweza kulamba asali nikawasaliti Watu ambao nimeteseka kwa miaka 30 kuwalinda”

“Nilisimama miaka 30 iliyopita kuitafuta haki nitasimama hapo kwa gharama yoyote, hakuna idadi ya fedha au mali itakayonifanya Mbowe niwasaliti Watanzania, nimepoteza Mabilioni ya fedha, anavyotokea Mtu anamuhukumu Mbowe eti amelamba asali, asali ipi?, nimezaliwa kwenye Familia yenye uwezo nimekua na kusimama kwenye Familia yenye uwezo lakini nimesema nitasimama na haki kwenye maisha yangu”