April 27, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Matumizi ya vilevi kwa mama mjamzito chanzo matatizo ya afya ya akili kwa mtoto aliye tumboni

Na Joyce Kasiki,Timesmajira,online,Dodoma

DAKTARI Bingwa wa Magonjwa ya akili katika Hospitali ya Taifa ya magonjwa ya Akili  Mirembe Dkt.Innocent Mwombeki amewaasa akina mama kuacha matumizi ya vilevi wanapokuwa wajawazito ili kuwanusuru watoto walio tumboni kuzaliwa wakiwa na matatizo ya afya ya akili.

Amesema,mama mjazito anapokunywa pombe anamuweka hatarini mtoto atakayezaliwa kuwa na matatizo hayo kwani kumsababishia  athari katika  ukuaji wa ubongo kwa mtoto aliye tumboni na hivyo kumsababishia tatizo la afya ya akili pindi atakapozaliwa.

“Tunapoangalia ongezeko la watu wenye matatizo ya afya ya akili,lazima tuangalie tangu mtoto anapokuwa tumboni,wapo akiana mama wengi wanatumia vilevi wanapokuwa wajawazito,hii ina athari kwa mtoto aliye tumboni.”amesema Dkt.Mwombeki

Dkt.Mwombeki ameyasema hayo jijini hapa leo kuelekea Oktoba 10 ambayo ni kilele cha  maadhimisho ya siku ya Afya ya Akili Duniani .

Akizungumza na waandishi wa habari kuhusu maadhimisho hayo amesema,mama mjazito anaweza kuwa chanzo cha kusababisha mtoto aliye tumboni kuzaliwa akiwa na matatizo ya afya ya akili.

“Mama mjamzito kutumia vilevi inasababisha ukuaji wa ubongo wa mtoto kuathirika na kusababisha mtoto kuzaliwa na matatizo ya afya ya akili na kuendelea kuongeza idadi ya wagonjwa wenye matatizo ya afya ya akiliu.ämesema Dkt.Mwombeki

Vile vile ametaja sababu nyingine inayosababisha matatizo ya afya ya akili ni pamoja na mtoto kutolishwa vizuri tangu anapozaliwa,kufanyiwa ukatili mbalimbali ,vipigo kwa watoto na manyanyaso mbalimbali.

Amewasihi akina mama wajawazito kuacha kutumia vilevi ili kunusuru afya za viumbe vilivyo kwenye matumbo yao.

“Pia kuna wale ambao wana vinasaba vya matatizo hayo katika ukoo,akipata changamoto kidogo tu katika maisha anajikuta anapata matatizo ya afya ya akili,lakini umasikini ,matatioz kazini yote hayo huchangia mtu kupata matatizo ya afya ya akili.ämesema Dkt.Mwombeki

Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi wa Magonjwa yasiyo ya kuambukiza kutoka Wizara ya Afya,Maendeleo ya Jamii,Jinsia,Wazee na Watoto,Shedrack Makubi amesema takwimu za Shirika la Afya Duniani (WHO) zinaonyesha  watanzania milioni saba wana matatizo ya afya ya akili huku akiutaja mkoa wa Dar es salaam  kuwa kinara kwa kuwa na watu wengi wenye matatizo ya afya ya akili kutokana na watu wengi matatioz hayo kwenda Jijini humo   kwa ajili ya kupatiwa matibabu.

Aidha watu zaidi ya milioni 300 wana matatizo ya afya ya akili duniani.

Mapema, Mkurugenzi wa Hospitali ya Taifa ya afya ya akili Mirembe,Dkt.Paul Lawale amesema wanakabiliwa na changamoto ya miundombinu ya hospitali hiyo kuwa chakavu kutokana na kujengwa wakati wa mkoloni  miaka 95 iliyopita.