April 24, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Magonjwa yasiyoambukiza yanavyoigharimu Taifa

Na Catherine Sungura,TimesMajira online

MAGONJWA yasiyoambukiza yanagharimu sana taifa na hivi sasa yanachukua maisha ya watu wengi na kwa rika zote.

Wizara ya Afya,Maendeleo ya Jamii,Jinsia,Wazee na Watoto imeona iwekeze jicho lake huko katika kupambana na magonjwa hayo ikiwemo kuhamasisha kwa kuwafikia wananchi waweze kujikinga na magonjwa hayo kwani yanaepukika. Moja ya magonjwa yasiyo ambukiza ni ugonjwa wa saratani.

Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii,walipotembelea Taasisi ya Saratani ya Ocean Road na kujionea Vifaa tiba vilivyopo pamoja na ujenzi wa mradi wa PET/CT Scan.

Saratani zipo za aina nyingi na hivi sasa magonjwa haya yameshamiri sana duniani na hivyo kuwaathiri watu wengi na kupelekea kuongezeka kwa vifo vitokanavyo na saratani duniani pote.

Katika kukabiliana na magonjwa hayo Serikali kupitia Wizara ya Afya imetenga shilingi bilioni 15.5 kwa ajili ya uwekezaji wa mradi wa ujenzi wa kituo cha kisasa cha kufanya vipimo vya saratani kwa kutumia teknolojia ya nyuklia (PET CT Scan) pamoja na kiwanda cha kuzalisha Mionzi dawa (radio Isotopes).

Serikali imeipa kipaumbee sekta ya afya ,uwekezaji huo utakuwa ni wa kihistoria wa kimakakati na kwamba utaiweka Tanzania kwenye dira ya kimataifa kwenye eneo la afya.

Mradio huo pia utasaidia watu wengi kupata huduma hizi za kibingwa kwa wakati kwani watu wengi walikua wakifika kupata huduma wakiwa kwenye hatua za mwisho.

Kiwanda hicho kitasaidia wananchi kuweza kujua hali zao mapema na uchunguzi utaonesha ugonjwa umeenea kiasi gani mwilini na hivyo kuifanya Taasisi ya Saratani ya Ocean Road (ORCI) kutambulika kwa mradi huo na kuwafanya nchi jirani kuja Tanzania kupata huduma hiyo.

Wakati wa ziara ya kutembelea miradi inayotekelezwa na Wiazra ya afya, kamati ya kudumu ya bunge ya huduma na maendeleo ya jamii iliyopata nafasi kutembelea mradio huo kwenye Taasisi ya Saratani ya Ocean Road jijini Dar es Salaam, Waziri wa wizara hiyo Dkt. Dorthy Gwajima anasema Taasisi hiyo imeendelea na uboreshaji katika eneo la miundimbinu ya utoaji huduma katika kipindi cha 2015-2020,Taasisi ilifanya uboreshaji katika maeneo mbalimbali.
Mradi wa PET/CT SCAN.

Dkt. Gwajima anasema taasisi ya saratani ya Ocean Road ina jukumu la kufanya uchunguzi wa ugonjwa wa saratani ili kuhakikisha inagundulika mapema, kujua hatua ya ugonjwa na kupata tiba sahihi.

Katika kufanya uchunguzi kwa mionzi, taasisi hutumia mashine za X-ray, Ultrasound na CT scan (radiology). Aidha, Taasisi unafanya uchunguzi kwa kutumia mashine ya gamma camera ikihusiksha dawa ya nyuklia anayowekewa mgonjwa ( Nuclear Medicine).

Mashine ya Gamma Camera ni mahsusi katika kuangalia uvibme kama ni wa saratani, kuangalia kama saratani imesambaa namna gani mwilini na pia inaangalia ufanyaji kazi wa viungo mwilini kama ubongo,tezi, figo, ini, moyo nakadhalika.Mashine hiyo hutumia teknolojia ya zamani ambapo walikua wanaingiza mionzi-dawa kutoka nje ya nchi (Afrika Kusini na uturuki) na hivyo kushindwa kufanya baadhi ya vipimo ambavyo ni muhimu kwa huduma za saratani.

Mashine ya kisasa ya teknolojia ya nuclear medicine ya kupima saratani mwilini Position Emission Tomography-Computerized Tomography sana(PET/CT scan).Mashine hii inahitaji mgonjwa kuwekewa mashine ya PET/CT ili kupimwa na kuangalia ugonjwa ulivyoenea mwilini hivyo ili huduma hii iweze kutolewa lazima kuwepo na vitu vifuatavyo.

Jengo la kusimika mashine husika na vyumba vya kuweka dawa za nyuklia kwa mgonjwa .Jengo hili lazima liwe na viowango ambavyo vinapitishwa na Tume ya Nguvu za atomiki Tanzania(TAEC) ili kulinda usalama wa wafanyakazi, wagonjwa na raia.

Mashine ya Cycloton hii ni mashine ambayo inazalisha dawa za nyuklia (radio isotopes) ambazo mgonjwa atapatiwa.Hiki ni kiwanda maalum cha kuzalisha dawa hizo.Mwisho ni lazima kuwepo na mashine ya PET/CT scan.

Dkt. Gwanima anasema mradi huo unahusisha ujenzi wa jengo maalum la kusimika mashine hizo maalum, maabara za kuchanganyia dawa za nyuklia na vyumba vya huduma pamoja na ununuzi wa usimikaji wa mashine ya Cyclotron na ununuzi wa mashineya PET/CT scan.

MANUFAA YA MRADI HUU

Mradi huu ukikamilika utakuwa na manufaa kwa Taifa katika utoaji wa huduma za uchunguzi na tiba kwa wagonjwa wa saratani ikiwemo kuboresha huduma za saratani nchini ziwe katika kiwango cha kimatifa hasa katika uchunguzi, kwani mashine hii ndiyo mashine ya kisasa kabisa katika uchunguzi wa saratani duniani kote.

Itasaidia kupunguza rufaa za nje na hivyo kuokoa fedha ambazo Serikali hugharamia wagonjwa nje ya nchi hasa India,hii ni ukweli usiopinga katika kuboresha sekta ya afya Serikali imekuwa ikiwekeza kwenye huduma bobezi ili kupunguza rufaa za nje ya nchi.

Utachangia utekelezaji wa sera ya serikali ujenzi wa viwanda kwani utahusisha kujenga kiwanda (cyclotron) ambacho ndiyo kitatumika katika kuzalisha mionzi-dawa (radio-isotopes) za upimaji katika PET/CT Scan.

Mradi huo pia utaongeza mapato ya taasisi kwani wagonjwa watalipia huduma za uchunguzi na hivyo kupunguza utegemezi wa ruzuku kutoka serikalini na pia kuongeza uwezo wa taasisi kugharamia shughuli za uendeshaji,kugharamia matengenezo kinga ya vifaa tiba ,ununuzi wa vifaa tiba na pia kugharamia stahili kwa watumishi na hivyo kuimarisha huduma za uchunguzi na tiba kwa wagonjwa wa saratani.

Aidha, mionzi dawa itauzwa kwa hospitali zingine hapa nchini na nchi jirani ambazo zitafunga mashine za PET/CT scan. Pia uuzaji wa mionzi-dawa utaongeza pia mapato kwa taasisi.

Kwa kuzingati kuwa PET/CT Scan haipatikani katika nchi za kusini mwa Jangwa la Sahara isipokuwa Afrika Kusini, hivyo kuwepo kwa kipimo hiki nchini kutavutia wagonjwa kutoka katika nchi za jirani ikiwemo Uganda, Kenya, Malawi, Msumbiji, DRC, Burudndi, Zambia, Rwanda, Comoro, Sudan ya Kusini na Somalia na hivyo kutekeleza kwa vitendo adhima ya Serikali ya kuimarisha utalii wa matibabu(Medical tourism).

Itakapokamilisha ujenzi huo Taasisi hii inakadiria kuwa itaweza kuhudumia takriban wagonjwa 2,000 kwa mwaka kutoka nje ya nchi, ambapo mapato ya wastani wa shilingi bilioni 3.2 kwa mwaka kwa huduma kwa huduma ya PET/CT Scan kwa wagonjwa kutoka nje ya nchi.Vilevile taasisi itapata mapato yatakayotokana na takriban wagonjwa 1,000 walio katika mfumo wa Bima ya Afya na wale binafsi hivyo kuingiza mapato ya takriban shilingi bilioni 1.6 kwa mwaka.

MALENGO YA TAASISI

Taasisi ya saratani ya Ocean road inayo malengo ya muda wa kati ambayo inalenga kuanzisha huduma za ubingwa bobezi katika tiba ya saratani kwa kupanua wodi za wagonjwa binafsi ili kuwa na uwezo wa vitandza 75 na kununua mashine ya tiba mionzi na MRI.

Kujenga kituo cha ubingwa bobezi cha huduma ya saratani katika eneo la Mloganzila na hospitali ya Rufaa ya kanda (MZRH) kwa utaratibu wa mashirikiano.,pamoja na kuanzisha huduma ya mionzi ya ndani ya saratani ya kooni katika njia ya chakula (esophageal cancer) kwa kupitia miradi ya ushirikiano wa Tanzania Comprehensive Cancer Project (TCCP).