April 29, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Maafisa ushirika toeni elimu kwa wakulima

Na Esther  Macha,Timesmajira,Online,Kyela

SERIKALI mkoani Mbeya imeagiza maafisa ushirika  kutoa elimu kwa wakulima wote  wanaojihusisha na kilimo cha zao la Kakao  katika wilaya za Rungwe , Kyela pamoja na Busokelo kuhusiana na mifumo  uuzaji wa mazao wa stakabadhi  ghalani   ili uendelee kumnufainisha mkulima  pamoja na kuogeza ubora wa zao hilo .

Kauli hiyo imetolewa jana na Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Juma Homera wakati wa mkutano wa wadau wa zao la Kakao ulioshirikisha wakulima wote wa halmashauri tatu zilizopo mkoani Mbeya ambazo zinajihusisha na kilimo hicho.

“Elimu hii itolewe kwa wakulima wote waliopo katika halmashauri zetu  tatu za wilaya za Kyela, Rungwe, pamoja na halmashauri ya Busokelo  lengo letu  tuone elimu hii inamfikia kila mkulima aliyeyopo kijijini ,apate elimu sahihi kuhusu uuzaji wa mazao wa stakabahi ghalani “amesema Mkuu huyo wa Mkoa.

Aidha Mkuu huyo wa mkoa alibainisha kwamba tozo za zao hilo  zilikuwa  na changamoto ya tozo zilizopitiliza ambapo kila  mkulima alikuwa akilipa shilingi.157  kama serikali wamepitisha maazimio  kuwa wananchi wanatakiwa walipwe kwa masaa 48 na kwamba baada ya mnada kufanyika wakulima wanatakiwa kulipwa fedha zao na kwamba anapochelewa kulipwa  mnunuzi anatakiwa kulipa faini ya shilingi .20 kwa kila kilo ambayo itakwenda kwa mkulima husika ambaye ana mzigo wake kwenye godauni.

Pia Mkuu huyo wa mkoa amesema kwamba katika mkutano huo pia wamefanya marekebisho ya tozo ambazo zilikuwa na fedha nyingi hivyo kama serikali imefuta tozo zote na mpaka leo hii mkulima badala ya kulipa shilingi .157  atatakiwa kulipa shilingi ,33 katika mnada wowote ambao utakuwa ukifanyika katika wilaya za Kyela ,Rungwe  na Busokelo  hivyo mkulima amepata punguzo la shilingi 125 kwa mahesabu ya kawaida mkulima ameondolewa fedha nyingi katika tozo hizo ambazo zilikuwa zinanyonya mkulima.

Akizungumzia kuhusu magunia mkuu huyo wa mkoa alisema kwamba waagizaji wa magunia walete magunia yenye ubora na kwamba kumekuwa kukiletwa magunia ambayo ndani yake yana  mabaki ya kahawa  na kusema hiyo ni hujuma kubwa kwa mfumo wa stakabadhi ghalani.

“Mfumo huo utaondoa watu wa kati upigaji na kwamba mtandao huo utasaidia usafirishaji au makuli ambao wanawalaungua wakulima pasipo kufuata sheria na taratibu”alisema.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa uendeshaji wa soko la bidhaa Tanzania (TMX)Augustino Mbulumi lengo la taasisi hiyo ni kumwezesha mkulima kuuza kwa ushinani zaidi na kwamba mnunuzi asilazimishe kununua kakao hadi wakubaliane soko la bidhaa.

“Lakini lengo letu pia ni kumwezesha mkulima auze zao lake kwa ushindani zaidi  badala ya kuuza kwa hasara ,taasisi yetu imekuwa msaada mkubwa kwa wakulima na tunaendelea kutoa elimu ili mkulima aweze kunufainika na kilimo na asione hasara kuingia kwenye suala la kilimo “ameema Mkurugenzi huyo Mbulumi.