May 12, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Lindi yavuka lengo uzalishaji wa ufuta

Na Said Hauni, TimesMajira Online, Lindi

MKOA wa Lindi umevuka lengo la uzalishaji zao la ufuta kutoka kilo 53,300,831 mwaka 2019 hadi kilo 62,284,032 mwaka huu na kuuwingizia maduhuri yenye thamani ya sh. 110,560,355,762/90, baada ya kuuza kupitia Vyama Vikuu viwili vya Lindi Mwambao na Runali.

Hayo yameelezwa na Mrajisi Vyama vya Ushirika mkoani hapa, Edmund Masawe wakati akiwasilisha taarifa ya utekelezaji kwenye kikao cha tathmini zao la ufuta, mbaazi na maandalizi ya msimu wa korosho mwaka huu.

Masawe amesema, kutokana na uzalishaji huo, mkoa umefanikiwa kuvuka lengo lililokuwa limejiwekea la kuzalisha kilo 59,500,000, hivyo kufanya ongezeko la kilo 2,74,032.

Amesema, makusanyo ya maduhuri hayo ni baada ya kuuza wa ufuta huo kupitia minada 17 iliyofanywa na Vyama Vikuu vya Lindi Mwambao, inayojumuisha Halmashauri za Lindi (Mtama), Kilwa na Manispaa, wakati Runali, inajumuisha Wilaya za Ruangwa, Nachngwea na Liwale.

Pia amesema, msimu wa mwaka 2020, mkoa ulilenga kuzalisha kilo 59,500,000 lakini kiwango hicho kimevukwa kulingana na hali ya hewa kuwa mzuri, ukubwa wa mashamba yaliyoandaliwa na wakulima kumesaidia kuongezeka kutoka kilo 53,300,831 mwaka 2019 hadi 62,284,032.

Mrajisi huyo amesema, Halmashauri ya Kilwa inaongoza kwa kuzalisha kilo 17,500,000, lakini hadi Agosti 31 mwaka huu uzalishaji umefikia kilo 17,161,129, ikifuatiwa na Liwale iliyozalisha kilo 12,413,488, wakati ilipanga kuzalisha kilo 12,000,000 na kuvuka lengo lililokuwa wamejiwekea.

Amesema, Nachingwea lengo lilikuwa kuzalisha kilo 7,500,000 na kufanikiwa kuzalisha kilo 10,300,321, Lindi (Mtama) kusudio ni kuzalisha kilo 9,000,000 na imezalisha kilo 9,072,777 huku Lindi Manispaa ikizalisha kilo 1,292,922, wakati lengo lilikuwa kuzalisha kilo 1,400,000.

Mrajisi huyo amesema, uzalishaji wa ufuta umekuwa ukiongezeka kila mwaka, ikilinganishwa na mwaka uliopita wa 2019, ambapo uzalishaji kimkoa ulifikia kilo 53,300,831.

Kwa upande wao wadau wakitoa michango yao kwenye kikao hicho, walilalamikia vifungashio, vikiwemo vya korosho na ucheleweshaji upatikanaji dawa za kupulizia miti ya mikorosho, mizani na kuchelewa malipo pale wanapokuwa wameuza mazao yao, ambapo Mkuu wa Mkoa wa Lindi aliwataka wafanyabiashara kuheshimu mikataba iliyowekwa.

%%%%%%%%%%%%%