March 29, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Kocha Man United alia na mwamuzi baada ya kipigo

MANCHESTER, England

KOCHA wa muda wa Manchester United, Ralf Rangnick ametupa lawama kwa mwamuzi Slavko Vincic kwa kuingia kwenye mtego wa Atletico Madrid, baada ya kikosi chake kutupwa nje ya michuano ya Ligi ya mabingwa barani ulaya hatua ya 16 bora baada kwa kukubali kichapo cha goli 1-0.

Ushindi wa bao 1-0 katika dimba la OLD Traford dhidi ya wenyeji wao Manchester United umetosha kuwafanya Atletico Madrid kufuzu hatua ya robo fainali kwa ushindi wa jumla wa mabao 2-1 kwenye michezo ya mikondo miwili. Goli la ushindi la Atletico lililowavusha kwenda hatua inayofuata limefungwa na Renan Lodi dakika ya 41.

Kufuatia matokeo hayo Kocha wa Manchester United Mjerumani Ralf Rangnick amemtuhumu mwamuzi wa mchezo huo Vincic kuingia kwenye mtego wa Atletico Madrid wa kupoteza muda, kocha huyo pia akahoji ni kwa nini ziliongezwa dakika 4 tu akitafsiri maamuzi ya mwamuzi huyo kutoka Slovenia kama ni ya kushangaza.

“Ilikuwa ngumu kipindi cha pili na kila mara mchezo ulisimama, mara zote wachezaji walikuwa wanajiangusha. Lakini pia nawezakusema baadhi ya maamuzi yalikuwa yakushangaza, sio kwamba hayakuwa muhimu lakini alihadaiwa sana na matukio ya kupoteza muda kwa kujiangusha na dakika nne za mwisho zilizoongezwa ulikuwa ni mzaha,” Amesema Ralf Rangnick.