May 19, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Kihenzile:NIT anzisheni vituo ukaguzi wa magari.

Na Penina Malundo, Timesmajira

NAIBU Waziri wa Uchukuzi, David Kihenzile ametoa wito amekitaka Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT) kuanzisha vituo vingi katika maeneo mbalimbali nchini kwa ajili ya kuongeza ufanisi katika ukaguzi wa magari.

Akizungumza Jana Dar es Salaam jijini Dar es Salaam , baada ya kutembelea miradi mbalimbali ya chuo hicho,amesema ni vema NIT kufungua vituo hivyo ili kusaidia kwa kiasi kikubwa kukagua magari kabla ya kuanza kutumika.

Anasema vituo hivyo vitaweza kusaidia kwa kiasi kikubwa kwa Taasisi za umma na binafsi kufanya ukaguzi wa magari yao katika vituo hivyo ili kupunguza matukio ya ajali.

“Ni wakati wa kutumia miundombinu hiyo kukagua magari kabla ya kuanza kutumika ili yawe na ubora,naelekeza mamlaka zinazosimamia vyombo vya usafiri kuhakikisha zinakaza nati kwa lengo la kunusuru maisha ya watu wasio na hatia na nguvu kazi ya taifa,” amesema Kihenzile.

Aidha akiongelea miradi mbalimbali ya Chuo hicho,Kihenzile amesema ni vema NIT kuhakikisha inakamilisha miradi yote kwa muda uliopangwa sambamba na kuhakikisha thamani ya fedha.

” NIT ongezeni hosteli nyingi ili kuchukua wanafunzi wengi na kupunguza changamoto ya wanafunzi kupanga nje ya shule ambako hakuna mazingira rafiki kwani idadi ya wanafunzi wanaongezeka sasa wamefikia 15,000 na wanatarajia kuwa wanafunzi wengi zaidi,”amesema.

Kwa upande wake, Mkuu wa Chuo Cha NIT, Prof. Zakaria Mganilwa amesema kituo cha ukaguzi wa magari kilijengwa kwa ajili ya wanafunzi wao, maofisa wa polisi wanaohusika na ukaguzi na maofisa wa bima.

“Tumekuwa tukihamasisha umma walete magari yao ili kujua ubora wake kwani tunakagua zaidi ya mifumo 15 hasa inayoendana na usalama wa gari,”amesema.

Profesa Mganilwa amesema watu ambao wanauziana magari wanawajibu wa kupeleka magari hayo kufanyiwa ukaguzi kabla ya kununua ili likaguliwe na watapewa taarifa ya gari husika.