May 5, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Kamati za Maamuzi matawi,kata chanzo cha rushwa za ngono kwa wanawake wanaowania nafasi za uongozi wa kisiasa

Na Rose Itono,timesmajira,online

KUTAWALA kwa vitendo vya rushwa ya ngono kwa Kamati za Maamuzi za baadhi ya vyama vya siasa ni kikwazo kikubwa kinachochangia wanawake wanaotaka kuwania nafasi za uongozi kipindi cha mchakato wa uchaguzi

Wakizungumza kwenye semina maalumu ya kujadili vikwazo wanavyokutananavyo wanawake wanaotaka kuwania nafasi za uongozi iliyofanyika mwishoni mwa wiki na kuratibiwa na Taasisi ya Sauti ya Jamii Kipunguni kupitia ufadhili wa Women Tanzania Trust Fund wamesema elimu inahitajika zaidi ili kuondoa vikwazo hivyo

Aisha Abdalah mmoja wa washiriki na mwanawake aliyewahi kuwania nafasi mbalimbali za uongozi kupitia ngazi ya siasa amesema vikwazo hivyo vinatengenezwa zaidi kwenye ngazi za Matawi na Kata

“Kamati za Maamuzi zinazopitisha zinazopitisha majina ya wagombea wa nafasi mbalimbali za uongozi ndani ya vyama ngazi za matawi na Kata ni vikwazo vinavyochangia kwa kiasi kikubwa vitendo vya rushwa ya ngono kwa wanawake wanaojitokeza kuwania nafasi, ” amesema Abdalah

Amesema endapo vyama vingekuwa vinawapatia elimu ya uongozi wanawake wanaojitokeza kuwania nafasi kabla ya mchakato huo kuanza vitendo hivyo vingepungua kwa kiasi kikubwa

Seya Kazadi mshiriki mwingine ambaye pia aliwahi kukutana na changamoto mbalimbali baada ya kujitokeza kuwania nafasi ya uongozi alisema elimu ya utoaji taarifa ya biashara ya vitendo hivyo ni muhimu sana kwa wanawake

” Wanadai rushwa ya ngono haina ushahidi, lakini ni dhahiri inaushahidi hivyo ipo haja kwa wanawake kupatiwa elimu ya namna ya utoaji taarifa kwa taasisi husika ikiwepo TAKUKURU juu ya viashiria vya vitendo hivyo,” alisema Kazadi

Ratifa Musa mkazi wa Chanika akichangia mada katika semina hiyo aliongeza kuwa mbali na vitendo vya rushwa ya ngonoi kuonekana kutokupendana baina ya wanawake kwa wanawake pia ni kikwazo kingine kinachofanya wanawake wanaowania nafasi mbalimbali kushindwa kusonga mbele

Amesema ubinafsi na majivuno yanayifanywa na baadhi ya wanawake mara baada ya kushika nyadhifa mbalimbali za uongozi ndiyo yanasababisha wanawake kutochaguana kwenye nafasi za uongozi

Aliongeza wanawake wengi mara baada ya kuchaguliwa wamekuwa wakijisahau na kujivuna pasipo kupigania haki za wanawake wenzao

Kwaupande wake Selemani Bishagazi ambaye ni Mkurugenzi wa Sauti ya Jamii Kipunguni ambao ndiyo waandaaji wa semina hiyo alisema watazifanyia kazi changamoto zilizoibuliwa

Amesema Sauti ya Jamii Kipunguni imeazimia kuendelea kutoa mafunzo hususan kutoa elimu kwa wahusika ngazi za Matawi na Kata huku akisisitiza kuwataka wanawake nchini kubadili tabia kwa kuacha kubaguana sambamba na kutoa taarifa za vitendo hivyo.