May 21, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Kalemani ashusha bei ya umeme kwa unit visiwani Mwanza

Na Mwandishi Wetu, TimesMajira Online, Mwanza

WAZIRI wa Nishati Dkt. Medard Kalemani amefanya Ziara katika kisiwa cha Maisome kilichopo Wilaya ya Sengerema jijini Mwanza na kuagiza kampuni binafsi ya Jumeme inayosambaza Umeme katika kisiwa hicho kutoza bei elekezi na Serikali ya Umeme Vijijini ya shilingi 100 kwa unit moja badala ya shilingi 2,000 mpaka 3,700 iliyokuwa ikitozwa na kampuni hiyo.

Akizungumza na wanakijiji wa kijiji cha Kanoni kisiwani Maisome, Waziri Kalemani ameeleza kuwa tayari Serikali imetoa bei elekezi ya umeme nchi nzima ambayo inasimamiwa na EWURA na ndio inayotumika na TANESCO katika kuuzia umeme wananchi hivyo ni vyema wawekezaji wote wakaifuata na kuizingatia.

Bei ya kuwauzia umeme wananchi ni moj ambayo inatumika na TANESCO na kusimamiwa na EWURA, hivyo naagiza Kampuni ya Jumeme iwashushie wananchi wa kijiji hichi bei na ifanane na ile inayotozwa na TANESCO katika maeneno mengine na huduma ziboreshwe, umeme usikatike mara kwa mara bila sababu za msingi” Alisema Waziri Kalemani

Waziri Kalemani ameendelea kwa kuagiza kampuni hiyo yenye ofisi zake jijini Mwanza kuhakikisha inafungua ofisi za kuhudumia wateja katika visiwa hivyo kwa huduma za dharura ili kuboresha huduma kwa wateja wanaohudumiwa na kampuni hiyo katika visiwa hivyo.

Naye Mwakilishi wa bodi ya Wakurugenzi ya kampuni hiyo ya Jumeme, Profesa Isack Safari, alipotakiwa kutoa maelezo ya utekelezaji wa agizo hilo, alieleza kuwa tayari wameanza kulifanyia kazi kwa kushusha bei ya umeme mpaka kufikia bei elekezi ya Serikali kama ilivyoagizwa pamoja na kubadilisha uongozi wa kampuni hiyo.

“Mheshimiwa Waziri, Kufuatia maelekezo yako uliyoyatoa mara kwa mara ya kututaka tuzingatie bei elekezi ya Serikali katika mauzo ya umeme tayar tumeyazingatia na hivi leo ulivyokuja kujiridhisha umekuta tayari tulishajipanga na tulishaanza kutekeleza maagizo hayo toka siku tutu zilizopita” amesema Profesa Safari.

Waziri kalemani amemalizia kwa kuiagiza TANESCO kuanza taratibu za kupeleka umeme wa gridi ya Taifa katika visiwa hivyo kwa kutumia Miundombinu inayopita chini ya maji ili kuwaondolea adha ya umeme wanayopata wakazi wa visiwa hivyo vilivyoko ziwa victoria vikilizunguka jiji la Mwanza.