April 19, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Jamii yaaswa kutowafungia watoto wenye ulemavu

Na Martha Fatael, Moshi

JAMII imeaswa kutowafungia ndani Watoto wenye ulemavu wa aina mbalimbali na kuwaona kama mzigo kwani wanafundishika na baadhi wanatibika wakiwa na umri chini ya miaka nane.

Hayo yamesenwa katika mahojiani maalum muuguzi wa kituo Cha malezi ya watoto wenye mahitaji maalumu Cha Faraja wilayani Moshi vijijini , Devota Mushi akizungumza na wanahabari wanawake mkoani hapa.

Amesema asilimia kubwa ya Watoto wanaozaliwa ama kupatwa na ulemavu katika umri wa chini ya miaka nane wanaweza kufundishwa kama ulemavu huo hautibiki na baadaye kujitegemea.

Aidha Mushi ametaka jamii kubadilika na kutowaficha watoto hao, kwani wanauwezo wa kusoma na kubadili maisha yao.

Kituo hicho ambacho kinalea watoto wenye mtindio wa ubongo na walemavu wa viungo, kimesema utafiti unaonesha watoto hao wanauwezo wa kusoma na kufanya shughuli za mikono.

“Jamii inapaswa kubadilika hawa watoto wanauwezo wa kusoma na wakaelewa, kujihudumia kama kula na shughuli nyingine ndogo ndogo za mikono, tusiwafiche” anasema.

Muuguzi huyo anasema kwa wale wazazi wanaokabiliwa na majukumu magumu ni vyema wakawapeleka watoto kwenye vituo ili wafanyiwe mazoezi na kujifunza.

Katika hatua nyingine, Mushi aliomba wadau kusaidia changamoto ya usafiri wa kuwapeleka Watoto hospitali kwani hutumia gharana kubwa kuwapeleka hospitali hususan nyakati za usiku.

Mapema baadhi ya wazazi Anna Msangi, Elimima Massao na Ally Mwenezi waliomba jamii kushirikiana na kituo hicho ambacho kimekuwa msaada kwao.

“Kituo hiki ni msaada kwa Watoto wetu hapo awali niliacha kazi ili niweze kumuhudumia ila kwa sasa anaweza kula, kuoga, anafua nguo zake mwenyewe ingawa kwa uangalizi””alisema Msangi

Hata hivyo mbunge wa Vunjo Dk. Charles Kimei alisema imekuwa ni utamaduni wa kawaida kusaidia vituo vyenye uhitaji kikiwemo hicho cha Faraja kwa vyakula na mahitaji mengine ya kawaida.

Awali, Katibu wa wanahabari wanawake Kilimanjaro, Mary Mosha aliomba wadau kwa kushirikiana na serikali ya kijiji kusaidia kituo hicho kipo Kwa maslahi ya jamii.

Aidha wanahabari hao wakiomba jamii kuamka na kufichua Taarifa za kufichwa kwa watoto hao ili Mamlaka husika zichukue hatua ili kuwanusuru.