May 19, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Isaya:Elimu ya uzazi muhimu kwa vijana

Na Penina Malundo, timesmajira

IMEELEZWA kuwa kuna umuhimu wa kutoa elimu ya uzazi wa mpango kwa vijana hasa wale wenye rika dogo ili kuweza kupunguza matokeo ya kupata wazazi waliochini ya miaka 18.

Akizungumza jana jijini Dar es Salaam,Nesi wa Kitengo cha Huduma za Uzazi wa Mpango wa Hospitali ya Palestina Sinza,Isaya Browno wakati wa ziara ya waandishi wa habari hospital hapo iliyoandaliwa na Chama cha Waandishi wa habari Wanawake (TAMWA)kwa lengo la kujifunza masuala ya haki ya afya ya uzazi amesema kuanza kutoa elimu hiyo ya afya ya uzazi kwa vijana imesaidia kwa kiasi kikubwa kusiwepo kwa mimba zisizotarajiwa nyingi.

‘’Sasa hivi hata vijana wanafika katika kituo chetu kupata huduma ya afya ya uzazi wa mpango bila kificho chochote na bado tunatoa elimu hadi katika mashule ambayo yamezunguka hospitali,’’amesema na kuongeza

‘’Miaka ya nyuma ilikuwa tofauti na sasa kwani vijana walikuwa hawapo tayari kupata huduma hizi ila miaka inavyozidi kwenda elimu ya afya ya uzazi inazidi kuwa inamuhimu kutokana na kuweka mazingira bora katika vituo mbalimbali vya huduma ya mama,baba na mtoto,’’amesema.

Amesema elimu hiyo utolewa hata kwa wamama ambao wametoka kujifungua wanaofika kliniki kwaajili ya huduma ya mama na mtoto ambapo uwapa ushawishi wa kutumia njia hizo za uzazi wa mpango..

Aidha amesema utoaji wao wa elimu ni kuondoa Imani potofu walizokuwa nazo watu wengi kuhusiana na njia za uzazi wa mpango kwani ikiwemo suala la kunenepa watu wanapotumia njia hizo,kupata mzunguko mrefu wa hedhi au wanakonda.

‘’Sisi tunampango dhabiti ambao tunatumia sisi kwenye kuweza kuondoa hizo hali kwa kuhakikisha mtu anapewa elimu kuweza kuelewa kwa kina,kuweka ukaribu kwa mteja pindi anapopata tatizo,’’amesema

Amesema kwa hospitali yao wateja wao wanaotumia njia za uzazi wa mpango wanachagua njia ya vijiti kuliko njia nyingine kutokana na elimu wanayopata.

Kwa Upande wake Muuguzi Mfawidhi katika Hospitali ya Palestina Sinza, Judith Katemba,amesema wamekuwa wakitoa ushawishi kwa wateja wao wanaoenda kupata huduma za kliniki ili kuweza kutumia njia hizo.

‘’Tunatoa uzazi wa mpango mama anapojifungua tunampa ushawishi wa kuanza kutumiaji wa njia za uzazi wa mpango ili kujikinga kutopata mimba zisizotarajiwa,’’amesema na kuongeza

‘’Pia tunahuduma rafiki kwa vijana lengo kuwakinga vijana wasipate mimba zisizotarajiwa na kutimiza ndoto zao,’’amesema.

Naye Mkuu wa Kitengo cha Miradi na Mikakati kutoka Chama cha Waandishi wa habari Wanawake (Tamwa) Sylvia Daulinge, amesema TAMWA inatekeleza mradi wa uhamasishaaji wa huduma za Afya ya uzazi wa mpango ili kuhakikisha wanawake na wasichana wanapata huduma hiyo.

Amesema wanawake na vijana wanapoelimishwa juu ya huduma hizo zinawasaidia kwa kiasi kikubwa kupanga uzazi wao na namna ya watoto wangapi wanahitaji .

“Tunashukuru uongozi wa hospital ya Palestina sinza kwa kutupa elimu ya masuala ya afya ya Baba,Mama na Mtoto , tunaamini kuwa mabalozi Wazuri katika kuelezea kwa jamii Kituo kinavyotoa huduma hii ipasavyo,”amesema.