May 16, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Dkt.Nungu:Wananchi tuwaunge mkono wabunifu

MKURUGENZI Mkuu wa Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknlojia (COSTECH)  Dkt.Amos Nungu  amewaasa watanzania kujivunia na kununua bidhaa zinazotengenezwa na wabunifu hapa nchini .

Akizungumza jijini Dodoma kwenye maonyesho ya wiki ya ubunifu Dkt.Nungu amesema,kumekuwa na dhana kwamba bidhaa zinazotengenezwa hapa nchini siyo nzuri jambo alilosema siyo kweli.

“Maonyesho haya yanaangalia ubunifu kwa upana wake ndiyo maana wananchi na wadau mbalimbali wanapaswa kuwekeza kwenye bunifu zetu kwani zinatengenezwa ili ziweze kutatua changamoto zilizopo katika jamii.”amesema Dkt.Nungu na kuongeza kuwa

“Tuache kasumba ya kudhani kwamba bunifu za hapa nchini kwamba hazidumu,dhana hii ndiyo inayofanya watu washindwe kununua bidhaa zinaotengenezwa na wabunifu wetu ambao tunawaandaa ili waweze kubuni na kutengeneza bidhaa zitakazowasaidia watanzania lakini pia zitaongeza ajira hapa nchini.”

Aidha amewaasa watanzani kujenga desturi ya kujitokeza kwenye maonyesho hayo ili waweze kujionea wenyewe bidhaa zinazotengenezwa na vijana wa kitanzania.

“Lakini tunaambiwa kwamba kuona ndiyo kuamini ,wananchi waanze kuthamini bidhaa zinazoundwa na watanzania na tuwaunge mkono lakini pia tutoe mrejesho kwa sababu ukishatumia ndio utatupa mrejesho kwa ajili ya kuboresha”

“Kwa hiyo tungetamani soko la ndani liweze kufanya kazi lakini tunategemea waandishi wa habari mlisemee hili ili wananchi wengi wapate taarifa kuhusu bidhaa zinazotengenezwa hapa nchini.”amesisitiza Dkt.Nungu