March 29, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

DKT Gwajima kuona wagonjwa

Na Mwandishi wetu, TimesMajira Online

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dkt Dorothy Gwajima ameanzisha mkakati wa kuzungumza na wagonjwa sambamba na ndugu wanaouguza wagonjwa hao katika vituo vya kutolea huduma za Afya hapa nchini kwa lengo la kusikia nini maoni yatakayotumika kuboresha huduma na kugusa matarajio yao.

Dkt Gwajima ameanzisha utekelezaji wa mpango huo katika Hospitali ya Taifa Muhimbili jijini Dar es salaam baada ya kupata malalamiko ya wagonjwa waliotuma ujumbe katika simu yake wakilalamikia baadhi ya huduma ambapo baada ya kufuatilia alibaini kuwa malalamiko hayo yangeweza kubainiwa mapema iwapo kungekuwa na utaratibu wa idara ya uhakiki wa ubora wa huduma kuongea na wateja wao na kusikia mrejesho wao.

Dkt. Gwajima alijichanganya na ndugu za wagonjwa kwenye eneo la wazi chini ya mti wa muembe ambapo ndugu hupumzika kusubiri saa ya kuingia kuona wagonjwa wao huku wengine wakiomba kuoiga picha na Dkt Gwajima wakimpongeza kwa utendaji wake mzuri.

Hali hiyo imewafurahisha wananchi kumuona waziri akitembelea wagonjwa na ndugu wa wagonjwa waliokuwa wakisubiri muda wa kuingia kuona wagonjwa ambapo wameipongeza serikali kwa kuboresha huduma za afya ikiwemo uwajibikaji wa watumishi, dawa na vifaa tiba licha ya kuwepo kwa changamoto kadhaa ambazo zimekuwa kero zikiwemo huduma za bima ya afya na vipimo kutakiwa kupima mara mbili kwa madai kuwa wataalamu hawana imani na vipimo vya hospitali alipotoka mgonjwa.

Kufuatia hali hiyo Dkt Gwajima ameziagiza Hospital zote kubwa kuanzia Hospital ya Taifa, Kanda na Mikoa kupitia vitengo vya ubora wa huduma kuanzisha vipindi vya kuzungumza na wateja kwa jina la Kigoda cha Mteja Tuzungumze kwa lengo la kupata maoni ya wananchi ili kuimarisha mifumo ya utendaji kazi.

Uongozi wa Hospitali ya Taifa Muhimbili Tayari umeanza kutekeleza Agizo hilo mara moja ambapo baadhi ya wananchi wanewasilisha maoni ikiwemo kuiomba serikali kuongeza watumishi ili wafanye kazi kwa ufanisi.