April 25, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Dkt.Gwajima awaagiza maafisa Maendeleo/Ustawi wa jamii kutoa elimu ya malezi na makuzi ya watoto kwa wazazi/walezi

Na Joyce Kasiki,Timesmajira,online,Dodoma

WAZIRI wa Maendeleo ya Jamii,Jinsia,Wanawake na Makundi Maalum Dkt.Dorothy Gwajima amewataka Maafisa Ustawi wa Jamii  katika Mikoa na Halmashauri zote nchini kuimarisha  utoaji wa elimu ya malezi na makuzi ya watoto kwa wazazi na walezi ili waelewe wajibu wao wa kulea watoto kwa kuzingatia misingi ya haki na usawa wa kijinsia.

Waziri Dkt.Gwajima ametoa agizo hilo leo wakati wa maadhimisho ya Siku ya Mtoto wa Afrika yaliyofanyika kitaifa mkoani Dodoma huku akisema lengo la kufanya hivyo ni kuwawezesha wazazi na walezi kulea watoto na kukua bila kuwa na vikwazo ikiwemo kufanyiwa vitendo vya ukatili.

Dkt.Gwajima amesema pamoja na jitihada mbalimbali zinazofanywa na Serikali za kukabiliana na vitendo vya ukatili kwa watoto, ikiwa ni pamoja na watuhumiwa wa ukatili kuchukuliwa hatua kali za kisheria, lakini bado kumekuwa na ongezeko la taarifa za vitendo vya ukatili wa aina mbalimbali dhidi ya watoto.

Dkt.Gwajima ameviytaja vitendo hivyo kuwa ni pamoja na Ubakaji, Ulawiti, Utumikishwaji wa watoto katika ajira hatarishi, Ukeketaji, Ndoa na mimba za utotoni na vitendo vingine vya ukatili.

Aidha kwa mujibu wa Takwimu za Jeshi la Polisi, Tanzania katika kipindi cha Januari hadi Desemba, 2021 jumla ya matukio ya ukatili kwa watoto yaliyoripotiwa katika jeshi la Polisi ni 11,499 ikilinganishwa na matukio 15,870 katika kipindi kama hicho mwaka 2020 (upungufu ni matukio 4,371 sawa na asilimia 27.5.

Akitaja mikoa iliyoongoza kwa vitendo hivyo vya ukatili dhidi ya watoto ilikuwa ni Arusha (808), Tanga (691), Shinyanga (505), Mwanza (500) na Mkoa wa Kipolisi Ilala (489). Aidha, makosa yaliyoongoza kwa idadi kubwa ni ubakaji (5,899), mimba kwa wanafunzi (1,677) na ulawiti (1,114).

“Kwa upande mwingine, utafiti wa serikali na UNICEF unaonesha asilimia 60 ya matukio yanatokea nyumbani na asilimia 40 yanatokea mashuleni. Tukumbuke, kuna uwezekano mkubwa kwamba matukio ya ukatili yanaweza kuwa mengi kuliko haya ukizingatia kwamba haya ni yale tu yaliyotolewa taarifa kwenye vituo vya polisi.”alisema Dkt.Gwajima

Hata hivyo amesema,katika kuongeza nguvu na kasi ya kupambana kutokomeza vitendo vya ukatili kwa watoto na kwenye jamii kwa ujumla, wizara kwa kushirikiana na wadau wake zikiwemo wizara mbalimbali za kisekta wanaratibu kampeni shirikishi ya jamii inayoenda kwa jina la Shujaa wa Maendeleo na Ustawi wa Jamii, 2022 (SMAUJATA).

Amesema dhana ya kampeni hiyo ni kuandikisha wanachama wengi zaidi kutoka ngazi zote na mitandao yote ya jamii wanaokerwa na uwepo wa ukatili, wenye moyo wa kujitoa bila ujira wowote kwenye kuelimisha jamii ili ifahamu juu ya uwepo wa ukatili na athari za ukatili na hatua gani wachukue kabla ya ukatili kufanyika na pale ambapo umefanyika.

Kwa upande wake  Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma za Maendeleo ya Jamii Stanslaus Nyongo amesema,wabunge wapo bega kwa began a serikali kuhgakikisha inatunga sharia ambazo zitamkinga mtoto dhidi ya ukatili.

Kwa upande wake mwakilishi wa Shirika lisilokuwa la kiserikali linalojikitaka katika kusaidiana na Serikali katika kutoa elimu juu ya stadi za malezi na makuzi bora ya watoto (ICS).

“Sisi kama ICS tunaamini msingi wa Taifa lolote imara na lenye nguvu kiuchumi ,kisiasa,kijamiina kiroho unaanza na malezi na makuzi bora na chanya ya mtoto kwani wao ndio Taifa la kesho.”

Awali akisoma risala kwa niaba ya watoto wote nchini ,Helen Masebo kutoka shule ya sekondari Bunge aliiomba Serikali kuhakikisha inaharakisha upelelezi wa kesi na kuchukua hatua kwa watuhumiwa wa ukatili dhidi ya watoto.