April 25, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Diwani Sultan azindua kampeni alama za usalama barabarani

Na Heri Shaaban, TimesMajira Online

DIWANI wa Upanga Mashariki, Sultan Salim kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo wamezindua kampeni za usalama barabarani Kata ya Upanga Mashariki.

Kampeni hiyo imezinduliwa leo katika shule ya Shaaban Robert iliyopo Wilayani Ilala ambapo Kampuni ya RockyandGlo Enterprise imepewa tenda ya kuchora alama za pundamilia ‘zebra crossing’ kwa ajili ya kupunguza ajali.

Akizindua Kampeni hiyo endelevu, Diwani Sultan amewapongeza wadau wa Upanga wakiwemo viongozi wa Shule ya Shaaban Robart kwa kufanikisha kampeni hiyo ambayo itakuwa ya Kata nzima ya Upanga Masharikiambayo ina shule saba za Msingi, tano za Sekondari na taasisi za Serikali na Vyuo.

Amesema, jukumu la kuweka alama za barabarani ni la Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) lakini wadau wamebeba jukumu hilo kwa lengo la kumsaidia ili kumuondolea kero kwa wapiga kula wake.

Pia ameitaka TARURA iweke kipaumbele maeneo ya vivuko vya shule kwa kuweka alama za usalama barabara ili kupunguza ajali kwa Wanafunzi.

“Nilipokuwa katika mkutano wa wananchi walielezea kero kutokana na kukosekana kwa alama za pundamilia maeneo ya shule kwani Kata yangu imezungukwa na shule za Msingi na Sekondari pia kuna kampuni ya kukamata magari ambayo imekuwa ikigeuza Kata ya Upanga Mashariki eneo la ATM kila wakati kukamata wapiga kula wetu” amesema Sultan.

Amesema, endapo kampuni hiyo itaendelea tena kuwakamata madereva basi atakula nao sahani moja kwani kwa muda mrefu wamekuwa wakifanya vitendo hivyo bila kifuata taratibu.