March 29, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

DC Mwanga aongoza mazishi mazishi ya Christopher Mfinanga

Mama mzazi wa Christopher Mfinanga, akiweka shada la maua wakati wa mazishi ya mwanaye yaliyofanyika jana katika makaburi ya familia kijijini Mangio, Vuchama, wilayani Mwanga. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu).

Na Mwandishi Wetu, Mwanga

MKUU wa Wilaya ya Mwanga, Tom Apson ameongoza mazishi ya aliyekuwa Mpigapicha wa Waziri Mkuu, Chris Mfinanga yaliyofanyika kwenya kijiji cha Mangio, Vuchama, wilayani humo.

Akizungumza na waombolezaji kijijini hapo jana, Mkuu huyo wa Wilaya ambaye alimwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Anna Mgwira amesema, Chris Mfinanga alikuwa mtu aliyejaa upendo ndiyo maana wengi wanahuzunishwa na kifo chake.

“Chris alikuwa mtu mcheshi na mwenye upendo, alisaidia wengi lakini tusisahau kwamba Mungu ndiye mtoa riziki. Msikate tamaa kwa sababu Mungu yupo na alimwezesha Chris na ndiyo maana aliweza kuwasaidia wengine na hata kuwasomesha watoto wenu.”

“Ninawasihi muamini kuwa Yesu yupo na kwake kuna faraja. Amini Yesu yupo na usiamini katika mganga wa kienyeji au ushirikina. Tuache ramli, tumtegemee Mungu nasi tutapata faraja,” amesisitiza.

Mapema, akiongoza ibada hiyo, Mchungaji Kiongozi wa KKKT Usharika wa Vuchama, Bill Graham Msangi amewataka waombolezaji waweke mambo yao sawa na Mungu wao pamoja na majirani wanaoishi nao.