April 25, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

DC Ilemela awafunda wazazi Kisiwa cha Bezi

Na Judith Ferdinand, TimesMajira,Online Mwanza

WITO umetolewa kwa wazazi wa watoto waliopo Kisiwa cha Bezi Kata ya Kayenze, wilayani Ilemela mkoani Mwanza kuendelea kuwatunza watoto wao katika misingi ya elimu.

Hayo yamesemwa na Mkuu wa Wilaya ya Ilemela, Hassan Masalla,wakati akizungumza na wananchi wa kisiwa hicho,wakati wa ziara ya kukagua miradi mbalimbali na kuzungumza na watu wa maeneo hayo.

Amesema,ni lazima kuweka nguvu ya kutosha ya kuwekeza katika elimu ili kutengeneza jamii iliyo bora. Alitoa wito kwa wazazi kuendelee kuwatunza watoto wao katika misingi ya elimu.

“Binafsi nawapongeza sana kwa jitihada kubwa ambazo mmezifanya katika upande wa elimu,tumepokea changamoto ya ukosefu wa nyumba za walimu, ni wajibu wetu kujipanga na kuanza kufanyia kazi mara moja,”alisema Masalla.

Sanjari na hayo,alimtaka Mtendaji awe muwazi wakati wa kusoma mapato na matumizi kila baada ya miezi mitatu na atoe ripoti ya matumizi na mapato.

Amesema pesa zinapokuja haachiwi mtu mmoja lazima iwe na maelekezo ya namna pesa ilivyotumika. “Lengo la kutoa pesa ni kuunga mkono jitihada za wananchi kwa sababu nimeona jitihada zenu katika miradi mbalimbali,”amesema Masalla.

Mkuu wa Wilaya ya Ilemela, Hassan Masalla akizungumzia na wananchi wa Kisiwa cha Bezi kilichopo wilayani Ilemela mkoani Mwanza,wakati wa ziara yake katika kisiwa hicho. Picha na Judith Ferdinand.

Aidha amesema hawawezi kuwa viongozi wa Serikali na kuwaacha watu wao wanapiga kelele, lazima washughulikie kero zao na kuzitatua.

Kwa upande wake Katibu wa Mbunge wa Jimbo la Ilemela, Dkt.Angeline Mabula, Kazungu Safari, amesema wameona misingi katika shule ya msingi Bezi,hivyo aliwahakikishia wananchi wa maeneo hayo kupitia Mbunge huyo watawapelekea matofali.

Kazungu amesema watoto wao wamemaliza darasa la saba hivyo wasiseme sasa wanayo elimu ya kuhesabu fedha na kuangalia kilo kwenye mizani.